0

wasaniii Tanzania  

Tasnia ya sanaa imekua, ukiachana na sanaa kama kivutio, kuna jingine kubwa na la msingi la sanaa kutengeneza ajira nyingi hasa kwa vijana na hapo hapo mtazamo wa sanaa umegeuka kuwa biashara.
Hili ni jambo la kushukuru sana kwa sababu sanaa inachangia kodi serikalini, hivyo kuwa moja ya vyanzo vinavyochangia maendeleo ya nchi, lakini wakati huohuo inaisaidia Serikali kupunguza tatizo la ajira kwa vijana.
Kusema ukweli kuna haja ya Serikali kuiangalia tasnia ya sanaa kwa jicho la pili ili kuiwezesha kupiga hatua, kwani imeshaonesha dhahiri jinsi ambavyo inaweza kushiriki kikamilifu katika kuchangia maendeleo ya nchi.
Sasa katika kuliangalia hilo kwa umakini kuna matatizo tayari yameshaanza kujitokeza miongoni mwa washika dau wa sanaa, na kama ulikuwa huwajui washika dau hao ni wasanii wenyewe na vyombo vya habari.
Unajua baada ya sanaa kukamilika, inahitaji mkono wa chombo cha habari ili iweze kutambulika kwa jamii. Hii ndiyo sababu washika dau hawa wawili wamekuwa mhimili mkubwa wa maendeleo ya sanaa nchini, kwa jinsi wanavyotegemeana katika kuendeleza.
Tatizo lililopo sasa, ni wadau hawa kuanza kuchukua upande katika mivutano inayoendelea nchini huku wadau wakiona dhahiri, jambo ambalo kwa majukumu waliyonayo, siyo sahihi.
Msanii ili awe mahiri, anatakiwa kuwa na mashabiki wengi na mara nyingi mashabiki hao huwa na imani tofauti za kidini na kisiasa na hutofautiana misimamo. Lakini wote hawa wanakuja kukutana kwenye sanaa baada ya kukubaliana na kazi za huyu msanii.
Hapo ndipo imani za kidini, kisiasa na nyinginezo huwekwa pembeni, watu wakakaa meza moja, kucheza muziki, ama kuangalia mavazi na wakati mwingine hata kuangalia sinema pamoja, huku wakiamini kwamba huyu msanii ni kwa ajili ya jamii nzima.
Lakini inapofikia mahali msanii huyu akaonyesha dhahiri imani yake katika siasa, ama dini na kuweka misimamo ya kuchukua upande fulani ndipo sanaa yake inapoanza kuingia doa kwani mashabiki ambao hayuko nao kwenye imani moja, lazima watagoma kukubaliana naye.
hapa ndipo wengi wanapoanza kupoteza mashabik na kuanza kuhisi pengine wanahujumiwa kumbe moto wameukoka wenyewe, kuukoka wanahisi utawaunguza.
Kila mwenye imani yake ataondoka na kurudi kule ambako anahisi kunamfaa, hali kadhalika na wanahabari wanayo changamoto hii.
Katika uandishi na utangazaji siyo vyema tukaonyesha dhahiri kwamba tumesimama kwa huyu, nasi pia tunasikilizwa na kusomwa na watu wa kila aina katika jamii.
Hata siku moja kuripoti kwetu hakutakiwi kusimama kwenye kutetea upande fulani. Tusimame kwenye kuipeleka taarifa kama ilivyo na kuichambua bila kulalia upande mmoja, mwishowe uamuzi tuwaachie wanajamii wenyewe waamue.
Ndugu zetu wanahabari iwapo mmejisahau, tunawakumbusha kwamba haya ni mambo ambayo mlifundishwa wakati mko vyuoni, kuhusiana na kusimama katikati ya jamii na kuripoti kilicho sawa na siyo kuweka misimamo yenu kwenye majukwaa mliyopewa.
Tunawatakia Jumamosi njema.

Post a Comment

 
Top