0

Wachezaji wa timu ya Yanga wakiwa mazoezini wakiwemo pia raia wawili kutoka nchini Brazil. Picha na Doris Maliyaga  

Dar es Salaam. Kocha wa Yanga, Marcio Maximo amewatetea nyota wake wawili kutoka Brazil, Andrey Coutinho, Santos Santana ‘Jaja’ kwa kusema ni wachezaji wazuri, na kama mnataka taarifa zao nendeni kwenye mtandao wa You Tube, mtaziona.
Kauli ya Maximo imekuja wakati wadau wa soka hususani mashabiki watani zao wa jadi Simba kubeza kuwa hakuna mchezaji mzuri kutoka Brazil akaja kucheza soka Tanzania ambayo soka bado linajikongoja.
Maximo alisema “Brazil kuna timu nyingi sana, na sio kila timu iliyopo kule ni kubwa, kuna nyingine zipo kama Coastal Union, naitolea mfano Coastal kwa vile naifahamu, na kule mpira unachezwa kwenye majimbo tofauti tofauti, kwa hiyo wasibeze ujio wao huku wakadhani ni wachezaji wabovu. “Wabrazili wengi wanaenda kucheza soka Angola, Angola wanaenda Brazil hata wachezaji wa Tanzania wanatakiwa kutoka kwenda kucheza soka Brazil, kama ambavyo Wakenya na Waganda wanakuja kucheza soka hapa Tanzania hivyo hivyo wachezaji wa hapa walitakiwa kwenda kule, lugha ya mpira inayoongelewa ni moja duniani hakuna tofauti.”
Pia, Maximo amewatema rasmi kwenye kikosi chake wachezaji Reliant Lusajo na Abuu Ubwa ambao awali aliwarudisha kundini.
Alisema kuwa aliamua kuwaita ili angalie uwezo wao kwa vile aliwafahamu viwango vyao miaka minne iliyopita, alitegemea vingekuwa vimepanda, lakini vimeporomoka.
“Nimeamua kuwaacha ili wakajipange upya, nisije nikawashikilia alafu baadae wakakosa timu za kuchezea, nimewachia waende kusaka timu wapandishe viwango vyao, Thabit Abdul amenivutia kiwango chake, kuna wachezaji chipukizi niliowaacha naona wanaendelea vizuri kama Omega Seme, nilitegemea Ubwa na Lusajo nao wangekuwa kwenye kiwango hicho, lakini bahati mbaya.” alisema kwa masikitiko Maximo.

Post a Comment

 
Top