0
Dodoma. Ligi Daraja la Kwanza ya netiboli inafikia ukingoni huku timu za Uhamiaji na JKT Mbweni zikishinda mechi zake walizocheza jana na juzi jioni na Polisi Kigoma na Polisi Shinyanga wakionekana kuvurunda kwenye ligi hiyo kutokana na kupoteza tena michezo yake.
Katika mchezo uliochezwa juzi, Uhamiaji iliwafunga Polisi Kigoma kwa mabao 46-9, JKT Mbweni ikashinda 36-13 dhidi ya Polisi Dodoma na kila mmoja kujiwekea matumaini ya kutwaa ubingwa wa michunao hiyo.
Mechi nyingine, TTPL iliwachapa vibonde wa ligi hiyo, Polisi Shinyanga kwa magoli 38-9, Polisi Morogoro ikatoa kipigo kwa ndugu zao wa Polisi Dodoma kwa magoli 20-17, Jeshi Stars ikaichabanga 37-21 Polisi Arusha na CIDT ikashinda kwa 18-29 dhidi ya CMTU.
JKT Ruvu walifanikiwa kuibuka na ushindi mbele ya Polisi Dar es Salaam wa magoli 37-21, JKT Mbweni ikawachapa tena Mbeya City 40-23, ambapo Polisi Mwanza ikawanyukwa na Polisi Dar es Salaam kwa magoli 23-18, huku JKT Ruvu wakiwagaragaza Polisi Shinyanga 47-3.
Hadi sasa michuano hiyo inaonekana kuwa mizuri kwa timu za Uhamiaji na JKT Mbweni, ambao wameonyesha kiwango kikubwa katika ligi hiyo, ambapo timu hizo zimepewa nafasi ya mmoja wapo kunyakua ubingwa wa mashindano hayo.
Kocha wa Uhamiaji, Winfrida Emmanuel alisema kasi waliyoianza haitaisha hadi mechi ya mwisho na hakuna timu ambayo inaweza kukwamisha, na kwa sasa mipango yake ya kunyakuwa ubingwa wa netiboli nchini inatimia.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Netiboli Tanzania (Chaneta), Anna Kibira alisema michuano ya mwaka huu imekuwa na ushindani mkubwa kutokana na viwango vikubwa vilivyoonyeshwa na timu shiriki haswa kutokana na kuwepo kwa vipaji vingi.

Post a Comment

 
Top