Dar es Salaam. Wakati msafara wa Tanzania ukiwasili kwenye
kijiji cha michezo tayari kwa michezo ya Jumuiya ya Madola nchini
Scotland, kocha mkuu wa timu ya taifa ya judo, Zaid Hamis ametoa kali
baada ya kueleza kuwa medali ya timu yake imebaki Tanzania.
Zaid aliyeambatana na wanajudo watatu kwenye
michezo ya Madola itakayofunguliwa Jumatano ijao kwenye Uwanja wa Celtic
Park jijini Glasgow, alisema: “Tegemeo langu kubwa la medali lilikuwa
kwa Ahmed Magogo, ambaye ameachwa Tanzania, hivyo medali ya judo
imeachwa nyumbani.”
Kocha huyo alisema anaamini Magogo ndiye
angeiletea nchi medali ya judo lakini kuondoshwa kwake siku moja kabla
ya safari kumemvunja moyo yeye pamoja na wanajudo wengine wanaoshiriki
kwenye michezo hiyo.
“Hii itanipa wakati mgumu kuwarudisha kwenye hali
ya kawaida wachezaji wengine, Magogo alikuwa bora zaidi,nilitegemea
medali ya Madola kutoka kwake, kama ningepata mbili basi moja ingekuwa
yake,” alisema kocha huyo.
Magogo alikuwa miongoni mwa wanajudo watatu
walioachwa baada ya taarifa zao kutoonekana kwenye Shirikisho la Jumuiya
ya Madola (CGF) nchini Scotland saa chache kabla ya ujumbe wa Tanzania
kwenye michezo hiyo kuondoka nchini, wachezaji wengine waliokumbwa na
dhahama hiyo ni Gervas Chilipweli na Amour Kombo.
Wakati huo huo, Katibu mkuu na Rais wa Kamati ya
Olimpiki Tanzania (TOC), Filbert Bayi na Gulam Rashid wanaondoka mchana
huu kwenda Scotland kwenye mkutano mkuu wa CGF.
Kwa mujibu wa Bayi, mkutano huo utafanyika
Jumatatu na Jumamnne kabla ya kushiriki sherehe za ufunguzi wa michezo
ya Madola, ambapo Tanzania inawakilishwa na wanamichezo 44 wa judo,
riadha, ngumi, kuogelea, mpira wa meza, kunyanyua vitu vizito na
baiskeli, huku Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe na Naibu Waziri wa
Michezo, Juma Nkamia wakitarajiwa kujumuika nao nchini humo.
Post a Comment