Msajili, Jaji Francis Mutungi.PICHA|MAKTABA
Tumesikitishwa na mgogoro kati ya Ofisi
ya Msajili wa Vyama vya Siasa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema), kiasi cha viongozi wake kudai ofisi hiyo inatumiwa na
wasaliti wa chama hicho kutaka kukivuruga. Kiini cha malalamiko ya
viongozi hao ni kauli iliyotolewa juzi na Msaidizi wa Msajili, Sistyl
Nyahoza kwamba mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe na Katibu Mkuu,
Dk Willibrod Slaa hawana sifa ya kugombea uongozi kutokana na kuzuiwa na
katiba ya chama hicho.
Msaidizi huyo wa Msajili alidai kwamba kipengele
cha ukomo wa mgombea katika Katiba ya Chadema ya mwaka 2006 kiliondolewa
kinyemela bila idhini ya mkutano mkuu, huku akisisitiza kuwa, Katiba ya
Chadema ya mwaka 2004 ilikuwa na kipengele cha ukomo wa madaraka wa
vipindi viwili vya miaka mitano. Kutokana na kauli hiyo, chama hicho
kimemtaka Msajili, Jaji Francis Mutungi kujitokeza na kueleza iwapo yeye
ndiye alimtuma msaidizi wake kutoa kauli hiyo.
Tunaposema tumesikitishwa na hali hiyo tuna maana
kwamba mgogoro huo ni mkubwa, ingawa baadhi ya watu wanaweza kudhani
unafaa kupuuzwa. Lakini yeyote ambaye amekuwa akifuatilia mwenendo wa
ofisi hiyo ya msajili tangu ilipoanzishwa kwa Sheria ya Bunge Namba 5 ya
mwaka 1992 atagundua kwamba, migogoro mingi iliyotokea katika baadhi ya
vyama vya upinzani na kuvivuruga, kwa kiasi kikubwa ilitokana na ofisi
hiyo kuwa sehemu ya migogoro kwa kuendesha shughuli zake kisiasa.
Sisi tulidhani kwamba uzoefu wa miaka 22 ya kuwapo
Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa ungetosha kwa mamlaka husika
kuhakikisha ofisi hiyo inakuwa mlezi wa kweli wa vyama vya siasa nchini.
Tofauti na mazingira ya kazi ya msajili aliyepo hivi sasa, mazingira ya
kazi ya wenzake waliomtangulia yalikuwa magumu mno kiasi cha wananchi
wengi kujenga dhana kwamba walikuwa mawakala wa chama tawala. Hivi sasa
dhana ya demokrasia na utawala bora imekubalika kwa kiasi kikubwa.
Hivyo, hatuoni kikwazo kinachoweza kumzuia msajili
wa vyama hivi sasa asifanye kazi kwa kujiamini na kutenda haki, kwa
maana ya kusimama kama mlezi na kutumia busara kufanya uamuzi kama
kiongozi wa vyama vyote vya siasa. Unahitajika umakini mkubwa kwa upande
wa msajili kutatua migogoro ndani ya vyama pasipo kuvuka mipaka yake,
kwani kinyume chake ni kuichochea. Hata hivyo, hatuna maana kwamba
msajili asihusike katika utatuzi wa migogoro. Tunachosema ni kwamba ni
muhimu kwake kwanza kufanya uchunguzi jadidi ili kufahamu ukweli kuhusu
pande zote zinazokinzana. Kukurupuka na kutoa hukumu kwa kusimamia hoja
za upande mmoja, tena kupitia kwenye vyombo vya habari ni kukuza tatizo.
Katika hili la Chadema, Msajili pia alipaswa
kusikiliza hoja za chama hicho kinachosema mwaka 2006 Katiba ya chama
hicho haikurekebishwa, bali iliundwa upya. Hoja ya Chadema kwamba
mabadiliko hayo siyo tu yaliridhiwa na mkutano mkuu Agosti 13, 2006 bali
pia yalipewa baraka na msajili aliyemtangulia, John Tendwa ni hoja
nzito ambayo ilipaswa kufanyiwa kazi ipasavyo. Pamoja na kwamba sisi
hatuna masilahi yoyote na upande wowote katika sakata hili, tungependa
kuweka wazi kwamba matamanio yetu pekee ni kuona mfumo wa vyama vingi
ukifanikiwa badala ya kuwa kiinimacho.
Post a Comment