Kwa mara nyingine Serikali kupitia viongozi na watendaji wake,
akiwamo Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), wamedai kwamba kiasi cha Dola
250 milioni za Kimarekani zilizopaswa kuendelea kuwapo kwenye ‘Tegeta
Escrow Account’ si mali ya Serikali na hivyo si mali ya umma.
Akaunti hiyo ilifunguliwa na Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini, Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) pamoja na kampuni ya Independent Power Limited (IPTL).
Akaunti hiyo ilifunguliwa na Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini, Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) pamoja na kampuni ya Independent Power Limited (IPTL).
Kwa bahati mbaya sana viongozi wa Serikali wamekuwa wakiendelea kurudia kuueneza huo uongo kwamba fedha hizo si mali ya umma.
Inasikitisha pia kwamba vyombo vya habari vimekuwa
navyo vikibeba na kusambaza huo uongo bila kuhoji na kuchunguza.
Inashangaza sana pia asasi za kiraia nazo zimekaa kimya. Inatisha na
kushangaza kuona wapinzani wakimwachia suala hili mbunge wa Kigoma
Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila, pekee wakati mapambano dhidi ya
rushwa ni ajenda kuu ya wapinzani.
Kafulila amekuwa akiendelea kuhoji suala hilo
bungeni peke yake bila kuungwa mkono na kupewa msaada wa aina yoyote
kutoka kwa wenzake wa kambi ya upinzani bungeni.
Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC)
ilielekeza kuwapo kwa ukaguzi maalumu kwenye akaunti hiyo ya escrow
iliyokuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kwa kuwa ndani yake kulikuwapo
fedha za umma.
PAC haina sababu yoyote ya kufuatilia fedha za
watu binafsi. Mwaka 2009 iliyokuwa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma
(POAC) ilitoa maelekezo kwa BoT kutothubutu kutoa fedha hizo. Agizo
hilo la POAC lilitokana na sababu kwamba fedha hizo zilikuwa ndani ya
hesabu za Tanesco.
Akaunti ya ‘Tegeta Escrow’ ilifunguliwa kutokana
na kuwapo kutoelewana kuhusiana na gharama halisi na halali za umeme
unaozalishwa na IPTL na kuuzwa kwa Tanesco.
Mahakama ya Usuluhishi ya Kimataifa (ICSID) katika
uamuzi wake wa Februari, 2014 ilitoa hukumu kuonyesha kwamba Tanesco
walitozwa kiwango cha juu zaidi ya kilichopaswa kulipwa kwa IPTL.
Kwa uamuzi huo ni dhahiri kwamba fedha zilizokuwa
zimehifadiwa kwenye akaunti hiyo maalumu zilipaswa kugawanywa kwa IPTL
na Tanesco baada ya hesabu kufanyiwa marekebisho upya kwa viwango
halali.
Hesabu za mwaka wa fedha ulioishia Desemba 2012 za
Tanesco, zinaonyesha wazi kwamba fedha hizo ni mali ya shirika hilo la
umma linalomilikiwa na Serikali kwa asilimia mia moja.
Fedha za kampuni ni suala la kisheria kama inavyobainishwa katika sheria ya kampuni ya mwaka 2002.
Kwa maelezo hayo na hoja hizo, inakuwaje Serikali ianze kudai kwamba fedha hizo siyo mali ya umma?
Hivi inawezekanaje fedha za mtu binafsi zikaingizwa katika
hesabu za shirika la umma linalomilikiwa na Serikali kwa asilimia 100?
Ni lini fedha hizo zimekoma kuwa za umma?
Serikali inadanganya waziwazi kudai kwamba fedha
hizo siyo mali ya umma. Umma una haki ya kukumbushwa kwamba madai hayo
yalitolewa pia katika lile sakata la ufisadi maarufu wa EPA unaofanana
kwa kila hali na huu wa sasa wa ‘Tegeta Escrow Account’.
Fedha zinazohusiana na akaunti ya escrow ni Dola
250 milioni za Kimarekani, kati ya hizo Dola 122 milioni zilizokuwa BoT
zimeshatolewa na kiasi kilichosalia Dola 128 milioni zitalipwa na
Tanesco kutokana na fedha zake kwa madai ya kushindwa kulipa kwa wakati.
Zitto Kabwe ni mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC).
Post a Comment