0
Utafiti uliofanywa katika sekta ya madini unaonyesha Tanzania ina aina 30 za madini. Ramani mpya ya madini kutoka wizara ya nishati na madini inaonyesha kuwa kila wilaya hapa nchini inakadiriwa kuwa na aina 30 za madini.
Hata hivyo, hali ya uchumi wa Tanzania na hali halisi ya maisha haifanani na watu wanaoishi katika nchi yenye madini na raslimali nyingi adimu kama vile madini ya dhahabu, almasi na tanzanite.
Aidha, miaka ya karibuni imegundulika uwepo mafuta na gesi, sekta ambazo zinaweza kuleta mapinduzi ya uchumi kwa Watanzania endapo viongozi watasimamia rasilimali hizo kwa uzalendo.
Maliasili tulizonazo za madini, gesi na mafuta iwapo hazitasaidia kutatua matatizo mbalimbali ya huduma za kijamii kama afya, elimu umeme na barabara bora ni sawa na nchi kuwa na laana kwa kuwa rasilimali zilizopo zikisimamiwa kikamilifu zinaweza kuleta maendeleo endelevu kwa Watanzania.
Bila kuwepo usimamizi madhubuti katika sekta ya madini, gesi na mafuta, wawekezaji wanaweza kumaliza madini yote na nchi itaendelea kubakia katika umasikini na kwamba madini yanaweza kubakia historia kwa vizazi vijavyo kwamba Tanzania ilikuwa na madini, yamekwisha bila kuwa na manufaa kwa nchi.
Ukiachia madini hayo, gesi asilia iligundulika kwa mara ya kwanza hapa nchini mwaka 1974 katika kisiwa cha Songosongo mkoani Lindi.
Ugunduzi wa gesi asilia umekuwa unaendelea katika eneo la bahari na inafikia takriban futi za ujazo trilioni 51. Pia kwa mujibu taarifa ya Shirika la Maendeleo ya Petroli nchini (TPDC) kuna uwezekano mkubwa wa kupatikana kwa mafuta katika maeneo mbalimbali nchini yakiwemo baharini na nchi kavu kwenye bonde ufa kama vile Ziwa Rukwa, Kyela na Bonde la Ruhuhu pamoja na maeneo mengine.
Tanzania inaweza kujifunza kutoka nchi jirani ya Uganda ambayo iligundua mafuta mwaka 2006 katika eneo la nchi kavu la Ziwa Albert ambalo ni mpakani mwa nchi hiyo na Kongo DRC .
Tangu kugundulika kwa mafuta hayo, Serikali ya Uganda imekuwa inafanya maandalizi ya kutosha na mwaka 2008 iliandaa sera, kanuni na kutunga sheria ya mafuta. Huduma za kijamii katika maeneo yaliyogundulika mafuta zimeanza kuboreshwa, hivi sasa kiwanda cha kusafishia mafuta kinajengwa katika wilaya ya Hoima ambayo mafuta yamegundilika.
Sekta binafsi katika nchi hiyo zimeshirikishwa na tayari wakulima 6,000 katika vijiji vilivyogundulika mafuta wamepata mafunzo maalum ya kuzalisha mboga na mifugo ya kisasa, ufundi na mafunzo ya ujasiriamali hata kabla ya uzalishaji wa mafuta safi kuanza.
Dennis Kamurasi, makamu mwenyekiti wa huduma ya jamii ya gesi na mafuta nchini Uganda, anasema sekta ya mafuta inatarajia kutoa ajira rasmi kwa watu 150,000 na ajira ambazo siyo rasmi zitakuwa zaidi ya 50,000.
Hapa Tanzania sekta binafsi zimechelewa kushiriki kuwaandaa wananchi ambao wapo katika maeneo ambayo yamegundulika kuwa na rasilimali kama mafuta na gesi hali ambayo imechangia kusababisha mgogoro na wawekezaji kama ilivyotokea mkoani Mtwara, hali iliyosababisha kutokea uvunjifu wa amani.
Wananchi hawajaandaliwa kupewa mafunzo mbalimbali kama ilivyofanyika nchini Uganda, ili waweze kutumia fursa hiyo kujipatia ajira ambayo sio rasmi kwa kuwa ni watu wachache tu ambao wanaweza kupata ajira rasmi.
Sera na sheria za mafuta pamoja na mikataba katika sekta ya madini, mafuta na gesi katika nchi ya Uganda ni ya wazi kila mmoja anaruhusiwa kuona, tofauti na hapa nchini ambako hadi sasa licha ya mikataba kutowekwa wazi, sheria ya gesi bado haipo licha ya mchakato wa uzalishaji wa gesi kuendelea.
Pia Tanzania inatumia sheria ya zamani ya utafutaji na uzalishaji wa mafuta ya mwaka 1980 ambayo iliandaliwa wakati wa siasa ya ujamaa na sasa haiwezi kukidhi mahitaji ya soko huria.
Bila kuweka vizuri sera, sheria za madini, mikataba, kanuni na kodi nchi husika haiwezi kunufaika na sekta hiyo ndiyo maana katika nchi ya Uganda licha ya mafuta kugundulika mwaka 2006 hadi sasa bado hawajaanza kuzalisha kwa sababu kwanza walimaua kuweka sera, kanuni na sheria ndipo waanze kuzalisha.
Kuzalisha mafuta na gesi bila kufanya maandalizi ya kutosha ni sawa na kuingia katika mashindano ya kunyonywa kwenye sekta ya gesi na mafuta hivyo kupoteza rasilimali ya nchi na kupora rasilimali za kizazi cha sasa na kijacho.
Albano Midelo ni mwandishi mwandamizi anayeandikia masuala ya maendeleo, madini, gesi na mafuta

Post a Comment

 
Top