0
London, England. Kiungo nyota wa klabu ya Manchester City, Yaya Toure amekataa ofa ya kujiunga na mahasimu wao wa mji mmoja, Manchester United.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Ivory Coast, Toure anadaiwa kutokuwa na furaha katika mji wa Manchester kutokana na sababu mbalimbali, ikiwamo klabu kushindwa kumtakia siku njema ya kuzaliwa na pia kushindwa kumpa ruhusa wakati mdogo wao alipokuwa hospitali kabla ya kufariki.
Inaonekana dhahiri kuwa nyota huyo wa zamani wa Barcelona ataondoka City, lakini kujiunga na miamba ya Old Trafford si chaguo lake.
Taarifa zinadai kwamba mabosi wa United wamekuwa wakifuatilia kwa ukaribu suala la kuondoka kwa Toure, ambapo wameweka mezani pauni 40 milioni kwa ajili hiyo, lakini Toure inadaiwa ameshawaambia kuwa hatarajii kujiunga nao.
Mchezaji huyo anadaiwa kuwa ana mpango wa kuondoka kabisa katika Ligi Kuu England, na huku mabingwa wa Ufaransa, Paris Saint Germain, wakipewa nafasi kubwa ya kumsajili.
Toure amekuwa mchezaji muhimu katika kikosi cha City na kukiimarisha katika Ligi Kuu, ambapo pia alimaliza msimu uliopita kwa kuipa City ubingwa wa ligi hiyo.
Toure ametwaa mara mbili tuzo ya mchezaji bora wa Afrika kutokana na kiwango chake kizuri uwanjani.

Post a Comment

 
Top