0
Dar es Salaam. Kocha mkuu wa Yanga, Marcio Maximo amesema atamka mshahara mchezaji yeyote atakayekwenda kinyume na matakwa ya timu.
Kocha huyo  jana alikuwa na kikao kirefu na wachezaji hao kabla ya kuanza kwa mazoezi ya timu hiyo, leo asubuhi kwenye ufukwe wa Coco na jioni watafanyia kwenye uwanja wa shule ya kimataifa ya IST Masaki.
Katika kikao hicho kilichoanza saa 2:30 asubuhi na kumalizika saa 4 asubuhi, Maximo alisisitiza suala la ushirikiano baina ya wachezaji na kukazia suala la nidhamu.
Maximo amewapa onyo wachezaji wote wa klabu hiyo kuwa atakayeonyesha utovu wa nidhamu atakatwa mshahara na hatakuwa na simile na mchezaji wa namna hiyo kwani  anasimamia falsafa yake kubwa ya kila mchezaji kujitolea kwa ajili ya timu na nidhamu nzuri.
Habari kutoka ndani ya kikao hicho ambazo Mwananchi imepata zilidai kuwa  Maximo aliwasisitizia wachezaji wake kushirikiana kwani ushirikiano ndio siri kubwa ya ushindi. “Nitakuwa nanyi kwa kipindi hiki, lakini  kubwa ninalopenda mimi ni nidhamu na ushirikiano baina yenu,  sitakuwa radhi kuona mchezaji anafanya vitu ambavyo haviendani na matakwa ya timu na yeyote akayefanya hivyo atakatwa mshahara.
Akimzungumzia kipa Kaseja ambaye walikuwa paka na Panya baada ya kukorofishana wakati akiinoa Taifa Stars, Maximo alisema sina tatizo na Kaseja, yaliyopita yamepita isitoshe hatukuwa na ugomvi, yale yalikuwa makubaliano, bila kuweka wazi alikuwa na makubaliano gani kati yake na kipa huyo.
“ Pia napenda kusisitiza kwenu kuwa sina ugomvi na kipa Juma Kaseja, yale yaliyopita yamepita na ilikuwa timu ya Taifa, lakini sasa tunaanza maisha mapya ili kuifanya timu hii itishe ndani ya nje  na kimataifa”alisema Maximo.Baada ya kumaliza kikao hicho Maximo alimuita  Kaseja na kukaa naye pembeni  na kuongea mambo mawili matatu ili kuwekana sawa.
Wakati huohuo; Kiungo wa Yanga, Nizar Khalfan ameponea chupuchupu kuondolewa ndani ya timu hiyo, huku kocha Marcio Maximo akitajwa kuwa ni sababu ya kumbakiza Jangwani.
Awali, Nizar alikuwa ni mmoja wa wachezaji waliopendekezwa kutemwa na kutolewa kwa mkopo, lakini ujio wa Maximo ukawafanya baadhi ya viongozi kufuta mawazo hayo na kumbakisha kiungo huyo wa zamani wa Mtibwa Sugar na Vancouver Whitecaps ya Canada.

Post a Comment

 
Top