0
Dar es Salaam. Wakati Mbeya City ikipangwa kufungua dimba la michuano ya kimataifa ya Bonde la Mto Nile dhidi ya El Merreikh Al Fasher Mei 23, kocha mkuu wa timu hiyo, Juma Mwambusi amesema wanakwenda Sudan kufanya kazi.
Mbeya City inaingia kambini leo kujiandaa na michuano hiyo itakayoanza Mei 22 kwenye viwanja vitatu tofauti nchini humo na Mbeya City iliyo kundi B itacheza mechi yake ya kwanza na  El Merreikh Al Fasher kwenye Uwanja wa Khartoum.
Akizungumza na gazeti hili jana, Mwambusi alisema nafasi waliyoipata walikuwa ‘wakiililia’ tangu walipopanda daraja kucheza Ligi Kuu hivyo hawatafanya mzaha na kuwaomba Watanzania kuwa pamoja nao.
“Tulitamani kumaliza ligi katika nafasi ya kwanza au ya pili ili tushiriki mashindano ya kimataifa ingawa tulimaliza kwenye nafasi ya tatu na sasa tumepata nafasi ya kushiriki mashindano mengine ya kimataifa huko tunakwenda kupambana,” alisema Mwambusi.
Kwa mujibu wa Mwambusi timu hiyo iliyokuwa ikijifua kwenye Uwanja wa Coca-cola na ule wa Shule ya Sekondari Iyunga mjini Mbeya.
Ofisa Habari wa Chama cha Soka Afrika Mashariki na Kati (Cecafa), Rogers Mulindwa alisema jana kuwa michuano hiyo itashirikisha timu 16 ambazo zitacheza katika hatua ya makundi na timu mbili katika kila kundi zitafuzu kucheza hatua ya robo fainali itakayoanza Mei 29 kabla ya fainali itakayochezwa Juni 4.

Post a Comment

 
Top