0

Kikosi cha Taifa Stars kikiwa nchini Gambia  
Leo timu yetu ya Taifa (Taifa Stars) itakuwa ugenini nchini Gambia kucheza na wenyeji wao katika mchezo wa kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia mwakani nchini Brazil.
Stars tayari imeishapoteza matumaini ya kufuzu kushiriki fainali hizo, lakini inatakiwa kucheza mechi hii dhidi ya Gambia kwa ajili ya kumalizia ratiba ya kundi C.
Katika kundi C timu ya Ivory Coast ndiyo inayoongoza ikiwa na pointi 13 ikifuatiwa na Morocco yenye pointi nane, halafu Taifa Stars ina pointi sita na Gambia inashika mkia ikiwa na pointi moja.
Tayari Ivory Coast imejihakikishia nafasi ya kusonga mbele kutoka kundi C kati ya makundi 10, ambapo kila kundi litatoa mshindi kucheza raundi ya tatu ambayo itatoa timu tano zitakazofuzu Kombe la Dunia 2014. Taifa Stars imeshindwa kupata nafasi ya kuongoza kundi C kwa kuwa haikufanya vizuri katika mechi zake.
Ilichapwa 2-0 na Ivory Coast ugenini, mechi ya pili iliichapa Gambia 2-1 nyumbani, ikaifunga Morocco 3-1 nyumbani Ikaja kupoteza kwa kipigo cha mabao 2-1 na Morocco ugenini na katika mechi ya tano, ilifungwa 4-2 na Ivory Coast.
Lakini pamoja na kushindwa kupata tiketi ya kufuzu kushiriki fainali hizo, bado tunaamini Taifa Stars wana jukumu la kuiwakilisha Tanzania na kucheza mechi hiyo dhidi ya Gambia kwa kujituma, uzalendo, umoja na na lengo moja ili kuipatia Taifa Stars ushindi.
Tunaamini wachezaji wamejiandaa vizuri na wataendelea kutekeleza wajibu wao wa kuliwakilisha taifa uwanjani bila kuidharau Gambia au kudharau mechi kwa kuiona haina umuhimu.
Mechi hii ni muhimu kwa Taifa Stars na Tanzania kwa jumla kwani kama tutashinda itatusaidia kumaliza katika kundi letu katika nafasi ya pili na hivyo kujiweka katika nafasi nzuri ya kupanda katika viwango vinavyotolewa na Shirikisho la Soka Kimataifa (Fifa) kila mwezi.
Hivi sasa Tanzania katika viwango hivyo vya Fifa inashika nafasi ya 128, wakati Gambia inashika nafasi ya 163.
Ni wazi Taifa Stars hawatakata tamaa, wanalipigania taifa letu kwa hali na mali, kujituma, kutengeneza nafasi nyingi za ushindi na kuzitumia. Watakuwa makini zaidi muda wote wa mechi huku wakiepuka makosa madogomadogo.
Wachezaji wa Taifa Stars wakiongeza umakini, wakitumia akili na kuwa watulivu uwanjani tunaamini wana uwezo wa juu wa kuleta matokeo mazuri uwanjani katika mechi dhidi ya Gambia.
Tunaamini, siku zote mchezaji wa timu ya taifa anachopigania ni ushindi kwa taifa lake, mchezaji wa timu ya Taifa anaposhinda huwa analiletea Taifa lake furaha na kujisikia fahari kuishi katika taifa hilo.
Hatutarajii wachezaji wetu wakate tamaa katika kuliwakilisha vizuri taifa lao, eti kwa sababu hata wakishinda mechi hiyo haitawasaidia.
Kwenye mapambano yoyote yale, suala la kukata tamaa linapaswa kuwa la mwisho mtu kulifikiria. Kukata tamaa mapema, maana yake ni kujipima haki ya ushindi.
Tunatarajia kuona wachezaji wa Taifa Stars wanaipa umuhimu mkubwa mechi hiyo kama ilivyokuwa katika mechi nyingine za hatua hii ya makundi.

Post a Comment

 
Top