Diwani wa viti maalumu manispaa ya Songea , Jacline Msongozi kushoto
akimuuguza Upendo Malembeka katika wodi namba tano alipolazwa baada ya
kupigwa, kubakwa na kung'atwa mdomo na sikio. Picha na Joyce Joliga
Licha ya Serikali, jamii na taasisi mbalimbali zikiwamo Chama
Cha Waandishi wa Habari Wanawake (Tamwa) na Kituo cha Sheria na Haki za
Binadamu(LHRC), kupiga vita ukatili wa kijinsia, baadhi ya watu wamekuwa
wakiendeleza vitendo hivyo huku waathirika wakiendelea kuwa wanawake.
Upendo Malembeka ambaye ni mkazi wa Mjimwema,
Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma ni mmoja wa waathirika wa vitendo hivyo
kwa kupigwa, kung’atwa mdomo, sikio na kubakwa na mwanaume ambaye hadi
sasa hajachukuliwa hatua zozote za kisheria.
“Kila nikikumbuka unyama niliotendewa machozi
yananitoka, sijui kwa nini aliamua kunitesa kiasi kile bila sababu.
Sijui nilimkosea nini hadi akaamua kunitendea hivi. Siju kwa kuwa ameona
mimi sina watu wa kunisaidia kutokana na umaskini wangu?
Naomba wanawake wenzangu na viongozi wa Serikali
wanisaidie ili haki itendeke, wanisaidie niweze kuangaliwa kama
nimeambukizwa Virusi vya Ukimwi kwa makusudi na kunipatia msaada wa
kisheria. Nina uchungu usiokwisha, kamwe sitasahau tukio hilo maishani
mwangu,” Upendo anaanza kueleza kwa uchungu akiongeza: Hivyo ndivyo
Upendo alivyoanza kusimulia mbele ya mwandishi wa makala haya huku akiwa
amenyofolewa kipande cha mdomo wa juu pamoja na sikio lake la upande wa
kushoto, kupigwa na kuumizwa vibaya machoni.
Upendo mwenye umri wa miaka 23 anaeleza kuwa
aling’atwa meno na mtesi wake na kubamizwa ukutani baada ya kugoma
kufanya mapenzi na mfanyabiashara wa maduka ya vifaa vya pikipiki
aliyefahamika kwa jina moja la Mwalongo.
Kisa hicho kimesikitisha wakazi wengi wa Songea
ambapo Upendo ameuomba uongozi wa juu , wanawake wenzake walio na uwezo
wa kumsaidia wafanye hivyo ili haki iweze kutendeka.
Akizungumza na kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa
wa Ruvuma, Wodi namba tano ambapo amelazwa, Upendo ambaye bado hali yake
ni mbaya kutokana na majeraha na maumivu makali anayopata anaeleza kuwa
bado hajafahamu hatima ya maisha yake kwa kuwa yeye hana uwezo wowote
zaidi ya kumtegemea Mungu pamoja na Diwani wa Viti Maalumu Jacline
Msongozi wa Manispaa ya Songea,ili amlipie matibabu yake na kumsaidia
fedha ya chakula na vitu vingine.
Akizungumzia tukio hilo Upendo anasema kuwa
alifika Songea mwaka 2007 akitokea Kahama mkoani Shinyanga katika Kijiji
cha Nyalwelwe kwa nia ya kufanya kazi za ndani kwa mwanamke aliyemtaja
kwa jina la Mama Komeka, ambapo baadaye aliamua kutafuta kazi ya uhudumu
katika baa.
Anasema: “Nakumbuka siku ya Agosti 25 mwaka huu
nikiwa nimemaliza muda wangu wa kazi ya uhudumu katika Pab ya Friends
iliyopo Songea, rafiki yangu ambaye pia ni mfanyakazi mwenzangu( Zai)
alipitiwa na mpenzi wake kazini hapo na kuniomba tuende wote disco,
lakini mimi nilikuwa sijisikii kwenda huko kwa siku hiyo nikamwomba Zai
aende mwenyewe.
Anasema kwa kuwa Zai alimwomba sana kwa madai kuwa hawatachelewa kurudi alikubaliana naye bila kujua yanayokwenda kumpata mbele.
Anasimulia kuwa wakiwa disko, shemeji yake
aliwanunulia vinywaji na kila walipomaliza aliwaongezea vingine, lakini
baadaye rafiki yake huyo akabadilika ghafla na kuanza kumnunia.
Anasema kuwa, wakati akiendelea kuwaomba
wamrudishe nyumbani alitokea rafiki wa shemeji yake, ambaye alikuwa
akizungumza na Zai mara kwa mara na kwa kuwa sauti ya muziki ilikuwa
kubwa, hakuweza kusikia walichokuwa wakizungumza.
Baadaye rafiki huyo wa shemeji yake alimfuata na kumweleza kuwa
asiwe na wasiwasi, watamrudisha au kumchukulia usafiri wa kurudi
nyumbani.
Upendo anaongeza kuwa kwa kuwa muda ulikuwa
umekwenda, alikwenda tena kuwaomba wamrudishe nyumbani na kuwakuta
tayari wameondoka, akawafuata nje ya ukumbi, ambapo baada ya muda
Mwalongo alimfuata akiwa ameshika Sh15,000 akimweleza kuwa wamekubaliana
wamchukulie chumba karibu na kazini kwake ili asubuhi ajihimu kazini
kwani muda ulikuwa umekwenda na ni hatari mtoto wa kike kutembea peke
yake usiku.
Anasema kuwa aliporudi ukumbini alikaa na kubaini
rafiki yake Zai na mpenzi wake wameshaondoka na rafiki wa shemeji yake
ambaye ndiye Mwalongo alimwomba amwamini na walikubaliana ampeleke
akalale.
Anaeleza kuwa alimpeleka nyumba ya wageni Mambo
Leo iliyopo Majengo na alipoulizia chumba na kukabidhiwa funguo
alishangaa Mwalongo akimwagizia pombe kwa mlinzi, lakini yeye alikataa
na kumweleza kuwa hahitaji pombe muda huo zaidi ya kutaka kupumzika.
“Wakati mlinzi akienda kumfuatia kinywaji,
nilishangaa kukabwa koo na kusukumiwa ndani, kisha kuzibwa mdomo na
kufungiwa ndani, huku nikitishwa kuwa iwapo nitapiga kelele atamuua,”
anasimulia kwa uchungu.
Anaongeza: “Nilipigwa na butwaa kuona nikishushiwa
kipigo na kuvuliwa nguo kwa nguvu, huku nikiingizwa vidole machoni kwa
lengo la kungolewa macho. Kipigo kilikuwa kikubwa na mfanyabiashara huyo
akaendelea kuning’ang’aniza tufanye mapenzi.
Sikuwa tayari, lakini Mwalongo aliniingiza bafuni
na kunigongesha kwenye ukuta wa choo, kisha kunimwagia maji mwilini,
kunisukumia kitandani na kuanza kunibaka bila ya kuvaa mpira wa kiume.”
Anasema kuwa Mwalongo hakuishia hapo, bali
aliendelea kumkaba na kumwambia kuwa akipiga kelele atamuua, ambapo
alishitukia ameng’atwa mikononi, kisha mdomoni na kutoa kipande cha
nyama ya mdomo wa juu.
Akieleza zaidi anasema kuwa ilipofika saa 11
alfajiri alimwomba Mwalongo amuruhusu aende kutibiwa hospitali kwani
maumivu yalikuwa makali, lakini aligoma na kumtaka amsubiri afuate pesa,
huku akiendelea kumtisha kuwa asipige kelele wala kumwambia mtu yeyote
kilichotokea.
“Nilikubali, lakini alipofungua mlango na kutoka
alinifungia chumbani, ndipo nikapiga kelele za kuomba msaada, ambapo
mmoja wa wahudumu aliwaeleza walinzi wamkamate mfanyabiashara huyo kwani
alikuwa amemjeruhi mtu vibaya. Walimkamata na kumpeleka polisi na mimi
kunipeleka hospitalini kupata matibabu, kwani nilikuwa na hali mbaya,”
anasema.
Kwa upande wa Diwani Viti Maalumu, Jacline
Msongozi amelaani tukio hilo na kusema kuwa ukatili aliofanyiwa binti
huyo ni wa kutisha na haupaswi kufumbiwa macho.
Ameviomba vyombo vya dola kumsaidia binti huyo ili
haki itendeke kwani tayari Upendo ameathirika kisaikolojia na amekata
tamaa ya maisha.
Msongozi anasema kuwa tabia ya wanaume kulazimisha mapenzi na
kubaka wanawake, imeshamiri mkoani humo huku waathirika wakubwa wakiwa
ni wanawake na watoto.
Diwani huyo amewataka wanawake kumsaidia binti
huyo ili kuvitokomeza vitendo hivyo na kuhakikisha wahusika wanafikishwa
katika vyombo vya sheria.
Aliongeza: Binafsi nimesikitishwa sana,
nimelifuatilia kwa kina tukio hili, nimekwenda polisi, naomba wampime
binti kujua kama ameambukizwa magonjwa, pia aliyefanya unyama huo
anafahamika ashtakiwe, Tuache kubebana na kuendelea kuumiza wanawake
kutokana na unyonge walio nao kwani hii siyo haki kabisa.”
Naye Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu
ameeleza kusikitishwa na kitendo hicho, ambapo ameagiza mtuhumiwa
aliyefanya kitendo hicho achukuliwe hatua za kisheria ili kukomesha
matukio ya aina hiyo.
Kwa upande wake Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya
Rufaa ya Mkoa wa Ruvuma, Dk Benedicto Ngaiza amekiri kumpokea Upendo
hospitalini hapo akieleza kuwa amepatiwa matibabu, hali yake inaendelea
vizuri na kwamba wanatarajia kumfanyia vipimo mbalimbali ili kubaini
iwapo ameambukizwa magonjwa.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma, Mrakibu
Mwandamizi wa Polisi, Revocatus Malimi amesema kuwa upelelezi kuhusu
tukio hilo unaendelea ambapo mtuhumiwa wa ukatili huo tayari amekamatwa
na polisi.
Post a Comment