0

 

Muziki ni miongoni mwa starehe inayomhusu mtu yeyote ikiweza kuburudisha, kufariji hata kuliwaza wakati wowote, popote kwa jambo lolote.
Ndivyo ilivyo kwani muziki huweza kutumika harusini, kwenye misiba na hafla mbalimbali ukisaidia kusherehesha, kufurahisha, kuomboleza, kuhuzunisha hata kumsifu na kumtukuza Mungu.
Lakini zaidi katika ulimwengu wa leo muziki ni zaidi ya  hayo hasa kwa vijana kwani umekuwa ni ajira inavyowavuta wengi kujaribu bahati zao kama watatoka kupitia fani hiyo.
Saidi Sekondo anayejitambulisha kwa jina la kisanii la ‘Saisalu’ ni mmoja wa vijana waliovutwa na fani ya muziki akijaribu bahati yake kutafuta riziki na mafanikio katika anayoyalenga.
Kwa malezo yake, Sekondo alianza muziki miaka tisa iliyopita ambapo ilikuwa mwaka 2005, lakini hadi kufanikiwa kutoa wimbo uliopigwa katika baadhi ya vituo vya redio, alitumia miaka saba kufanikisha hilo ambapo mwaka 2012, alitoa wimbo wake wa kwanza alioupa jina la ‘Kipato Kidogo’.
Saisalu anasema kuwa wimbo huo alimshirikisha mwimbaji Steve RnB, mtayarishaji akiwa na Man Water kutoka Studio za Combination Sounds.
Hata hivyo anasema kuwa kwa bahati mbaya video ya wimbo huo haikuchezwa sana kutokana na kuwa na picha isiyovutia.
Anasema kwamba kwa sasa ana wimbo mpya unaokwenda kwa jina la ‘Madikodiko’, aliourekodi Studio za Mazuu na kwamba umeanza kuchezwa kwenye baadhi ya vituo vya redio.
Saisalu anaeleza kuwa pamoja na kuvutiwa na wanamuziki wengi wa miondoko ya Bongo Fleva, hakuwaza kujiingiza huko kwa ajili ya kufuata wanachokifanya, bali kuja na mitazamo tofauti na kufanya kitu tofauti.
“Nilikuwa nawasikiliza waimbaji wa Bongo Fleva walio na mafanikio, pia  chipukizi kama mimi nikagundua uwezo wa kufanya kitu kama wanachofanya wao ninao, hivyo baada ya kumaliza masomo yangu ya ufundi mwaka 2005 nilianza harakati rasmi, “anasema Saisalu.
Anabainisha kuwa katika sanaa yake nyimbo zote anatunga mwenyewe na kwamba sasa anahitaji nyimbo mbili ili kukamilisha albamu yake itakayokuwa na nyimbo saba.
Anataja nyimbo zake kuwa ni pamoja na kwanza wa ‘Kipato Kidogo’, Madikodiko ulio kwenye asili ya mdundiko, Sjachoka kusubiri, Mgumba, na Mtetea zikiwa katika miondoko ya Bongo Fleva.
Anaeleza kuwa licha ya kuwapo kwa changamoto nyingi ikiwamo baadhi ya madj kudharau kazi za wasanii chipukizi kwa kuacha kwa makusudi kuzipiga katika vituo vya redio bado hajakata tamaa.
Saisalu anasema kuwa alichojifunza ni wasanii wengi walifanikiwa kwa kupata watu wa kuwashika mkono hivyo kupata fedha za kurekodi kwenye studio bora na kupata matangazo kwenye vyombo vya habari jambo analolitaja kuwa ni tatizo kubwa kwa wasanii hasa wachanga akieleza kuwa bila kujulikana hata msanii akiwa na kazi nzuri vipi ni kazi bure.
“Baadhi ya redio zinarudisha nyuma kutokana na kupiga nyimbo za wasanii wenye majina. Sisi wachanga, kama unataka nyimbo yako ipigwe basi uwe na kitu kidogo, ingawa zipo baadhi zinazotupa sapoti na zibarikiwe sana, “anasema Saisalu.
Anasema pamoja na hayo yote tayari ameshajisajili kwenye Baraza la Sanaa Tanzania (BASATA).
Kuhusu elimu anasema kuwa alisomea ufundi wa kutengeneza viyoyozi katika Chuo cha Ufundi (VETA) ngazi ya cheti kutokana na ufundi huo kuhitaji elimu zaidi ameamua kuwekeza nguvu na akili katika muziki akiamini atapata fedha za kuongeza ujuzi wake.
Anaeleza kuwa elimu aliyonayo haimwezeshi kuingia kwenye soko la ushindani kwani kila siku vifaa vya umeme vinakuja vipya na kuhitaji ujuzi zaidi.
“Naamini nikiwa na ujuzi zaidi ni rahisi hata kufungua kampuni na kupokea zabuni za matengenezo ya vitu mbalimbali. Kama nitafanikiwa katika muziki, cha kwanza ni kuongeza ujuzi, “anasema Saisalu.

Post a Comment

 
Top