0
Dar es Salaam. Safu ya ushambuliaji ya Simba imeimarika baada ya kumsajili mshambuliaji wa Ruvu Shooting, Elias Maguli pamoja na kuwasili kwa kiungo Mrundi Pierre Kwizera (23) jana mchana.
Maguli amesaini mkataba wa miaka miwili jana mchana na sasa anatengeneza kombinesheni na Mrundi Amisi Tambwe katika safu ya ushambuliaji.
Maguli msimu uliopita alifunga mabao 14 na kukamata nafasi ya pili katika orodha ya wapachika  mabao nyuma ya Tambwe aliyefunga mabao 19.
Maguli alisema, anajisikia furaha kujiunga na Simba, kwa vile ni miongoni mwa timu kubwa na kongwe hapa nchini.
“Nimesaini mkataba wa miaka miwili leo ya kuichezea Simba na bila kuficha nina furaha kujiunga na timu hii kwani ni timu kubwa hapa nchini.
“Najua kuna changamoto kuichezea timu kubwa kama Simba lazima nipo tayari kukabiliana nazo na kuzishinda,” alisema Maguli.
Aliongeza: “Nitajitahidi kadri ya uwezo wangu kutoa mchango utakaosaidia timu kupata mafanikio.”
Msemaji wa Ruvu Shooting, Masau Bwire alilithibitishia gazeti hili kwamba klabu yake imemalizana na Simba na kumruhusu Maguli kuanza maisha mapya.
“Natangaza rasmi kwamba Maguli sasa ni mali ya Simba baada ya taratibu zote kufuatwa kwetu hatuna kingine cha kusema zaidi ya kumtakiwa kila la kheri.”
Kwizera aahidi mataji Simba
Kiungo Mrundi, Pierre Kwizera (23) ametua nchini jana saa nane mchana akitokea  Ivory Coast katika klabu ya Afad na kuwaahidi mashabiki wa Simba kuwa amekuja kuleta ubingwa.
Kiungo huyo alisema, “Nimekuja kuwapa ubingwa Simba na kazi yangu kubwa ni kuhakikisha ushindi unapatikana na timu kupata mafanikio.
“Mimi ni kiungo mkabaji, lakini nakuja na kitu cha tofauti ambacho ni kuwa nina uwezo wa  kucheza mipira mirefu na pia kufunga kwa faulo. Kwa sasa ninachooomba ni ushirikiano ili niweze kuzoea mazingira. Nataka kucheza Simba kwa mafanikio na kwa kuangalia mafanikio ya timu zaidi,” alisema Kwizera.
Ujio wa kiungo huyo kwenye kikosi cha Simba, unakamilisha nafasi za wachezaji wa kigeni kwenye klabu hiyo ambayo inatakiwa kuwa tano.
Wachezaji wengine wa kimataifa waliopo Simba ni Amisi Tambwe (Burundi),  Paul Kiongera (Kenya), Donald Musoti (Kenya ) na Joseph Owino (Uganda).

Post a Comment

 
Top