0

Baadhi ya wakulima walipinga wakisema ipo kampuni inayonunua pareto yao kwa Sh2,200 na kulipa papo kwa papo na kwamba pia wapo watu waliofika kwenye vijiji kuwataka wakulima wasilime pareto.PICHA|MAKTABA  

Mbeya. Wakulima wa Pareto mkoani hapa wamehoji uwapo wa mkanganyiko wa bei ya zao hilo msimu huu baada ya kuwapo kwa wanunuzi wanaowalipa Sh2,200 papo kwa papo huku wengine wakiwalipa Sh1,500 kwanza na nyingine hulipwa baada ya kupima sumu.
Malalamiko ya mkanganyiko huo waliutoa mbele ya Ofisa Kilimo wa Kampuni ya Pareto Tanzania (PCT), Christopher Shimwela aliyefika katika Kata za Maendeleo na Itala Mbeya Vijijini kwa ajili ya kuwafafanulia bei ya pareto kwamba ni kati ya Sh1,500 na Sh2,5000 kutegemeana na ubora na uwingi wa sumu.
Shimwela alisema bei ya pareto kwa kawaida ni kati ya Sh1,500 hadi 2,500 kwa kilo moja lakini mkulima alipwe kwanza Sh1,500 ambazo ni sawa na bei ya pareto yenye sumu chini ya asilimia 0.9 na kwamba fedha nyingine watalipwa ndani ya siku 30.
‘Kwa mfano wakulima wa Vijiji vya Uzaha Muungano walilipwa Sh1,500 kwa kilo baada ya kuuza pareto yao lakini baada ya kupima pareto yao imekuwa na sumu ya asilimia 1.4 hivyo wataongezewa Sh700 kwa kila kilo’’ alisema.
Hata hivyo, baadhi ya wakulima walipinga wakisema ipo kampuni inayonunua pareto yao kwa Sh2,200 na kulipa papo kwa papo na kwamba pia wapo watu waliofika kwenye vijiji kuwataka wakulima wasilime pareto.
Akizungumzia utata huo, Mkurugenzi wa Bodi ya Pareto Tanzania, Ephraem Mhekwa alisema mnunuzi yeyote atakayenunua pareto na kuwalipa wakulima zaidi ya Sh1,500, atanyang’anywa leseni.
Mhekwa alisema wanunuzi wote wanatakiwa kuwalipa wakulima kwanza Sh1,500 na kwamba kiasi kingine wawalipe baada ya kupima uwingi na ubora wa sumu ndani ya siku 30.
Mhekwa alisema kampuni itakayovunja sheria na kanuni za ununuzi wa pareto msimu huu itafutiwa leseni mara moja na kwamba Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Kilimo , Chakula na Ushirika ilishaagiza kila mununuzi awalipe kwanza wakulima Sh1,500 na baada ya kupima ubora wa sumu wawalipe tena malipo ya pili.

Post a Comment

 
Top