0
Mathalan Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kimekuwa kikishika nafasi ya nne kwa ubora wa elimu kwa miaka kadhaa sasa miongoni mwa vyuo vikuu bora 100 barani Afrika. Je, nafasi hii itaendelea kutetewa na chuo kinachoiwakilisha nchi kwa miaka michache ijayo?
Kubwa zaidi ya yote, taaluma ya ualimu ni taaluma ya ajabu yenye sifa bainifu miongoni mwa taaluma nyingine, achilia mbali suala la kutokuwa na mipaka inayoweza kuonyeshwa kwa urahisi kwa taaluma.
Ninavyofikiri mimi, asili ya ualimu ni suala la kiroho. Kufundisha ni zaidi ya kile kinachofikiriwa na watu wengi; kitendo cha mwalimu kusimama mbele ya wanafunzi darasani na kuwafunza yale masomo yaliyopangwa. Hata hivyo ili hilo lifanyike kwa ufanisi linawezeshwa na uwepo wa hali fulani ndani ya mwalimu.
Hali hii ndiyo humwezesha mwalimu kuwa tayari, huru na aminifu (genuine) kutoa kile kinachotakikana kwa maendeleo ya ubongo wa mwanafunzi. Kwa kuwa kazi kuu ya mwalimu ni kumsaidia mwanafunzi na kumpa mwelekeo fulani, kunahitajika umakini wa hali ya juu sana ambao utategemea hali aliyo nayo mwalimu.
Huu ndiyo uamilifu mkuu wa mwalimu kwa jamii kwamba ni kulea na kumpa mwelekeo ubongo au tunu za asili za mwanafunzi (mwanadamu). Hivyo kama mchakato na kanuni hii vikikosewa tayari mtoto / mwanafunzi atafuba.
Ndiyo maana utasikia watu wengi wakilalamika kuwa siku hizi watoto hawafundishwi sawasawa, walimu hawatekelezi wajibu wao sawasawa. Anayeijua siri ya urembo ni mwalimu. Mhadhiri wangu mmoja siku moja alionyesha hisia zake juu ya mwenendo wa elimu nchini wakati alipokuwa anatoa somo alisema kuwa ana uhakika miaka 50 ijayo hatokuwa hai ili ashuhudie taifa la ajabu ambalo watu wote hawatakuwa tena na uwezo wa kiakili tangu viongozi wao hadi watoto wadogo. Kwa sababu kanuni za elimu zimekiukwa.
Madhara mabaya ya elimu ( walimu) hayaonekani kirahisi kwani yanafanya kwa mbinu za hali ya juu sana. Ni mchakato unaofurukuta chinichini. Ukifikia hali ya kuonekana waziwazi haiwezekani kirahisi kuzuilika ambapo vizazi kadhaa itakuwa vimekwisha haribikiwa tayari. Ni suala la ndani la kisaikolojia. Tiba yake ni kutibu saikolojia ya mwalimu na wala sio kumtishia au kugombana naye.
Na mara nyingi mtu anayejiamini kuwa na madhara makubwa si mpigaji wa kelele sana. Akisema ukweli atapingwa anachokifanya anakaa kimya na kutekeleza uaminifu wake. Jambo hili pia linakwenda nje ya uwezo wa uzalendo alionao. Ni nguvu ya ndani mwake.
“Unafikiri ni nani kati ya daktari na mwalimu ana madhara makubwa na mabaya zaidi akitoweka katika jamii?” elimu ni uwanja mpana sana ambao si rahisi kuuzungumzia kwa wakati mmoja.
Kwa dhana hiyo utakubaliana na mimi kuwa ‘UHAI WA TAIFA LOLOTE UMO MIONGONI MWA MWALIMU’. Mwalimu ni kundi la watu ambaolo ndilo huamua tabia na mwelekeo wa Taifa lolote”.
Hivyo ningeshauri kuwa suala zima la elimu ndani liachiwe kwa wadau husika, walimu wakiwa ndio kiini cha suala hili. Serikali na vyombo au wadau wengine wabaki kuwa wawezeshaji wa wataalamu hawa, ili watekeleze wajibu wao kwa furaha na waaminiwe kwani ndio waliopewa wito huu muhimu wa kuandaa taifa.
Walimu nao kwa upande wao wautafakari wito wao vema.
Ninalopenda kusisitiza ni kwamba; ualimu usitafsiriwe kama kazi yakuhamisha ujuzi alionao wa masomo kama Hisabati, Kiswahili nk.
Mwandishi ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Anapatikana kwa simu 0752 – 480824

Post a Comment

 
Top