0
Dar es Salaam. Serikali imesema imefanikiwa kudhibiti matumizi yasiyofaa ya tindikali baada ya kuweka utaratibu unaowaruhusu watu walioorodheshwa tu kununua kemikali hiyo.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Mkemia Mkuu wa Serikali, Profesa Samwel Mnyele alisema utaratibu mpya wa kuzuia kila mtu kuuziwa tindikali umesaidia kupunguza matumizi mabaya ya kemikali hiyo.
Wakala wa Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA) uliandaa utaratibu wa kuhakikisha watu wote wanaotumia tindikali kwa ajili ya shughuli mbalimbali wanaorodheshwa.
“Tulihakikisha watu mbalimbali, wakiwamo wanaotoa elimu ya ujasiriamali wa kutengeneza sabuni na bidhaa nyingine, wanajiorodhesha,” alisema.
Alisema wakufunzi ndio wanaouziwa tindikali hiyo na wao wanaigawa kwa walengwa.
Alisema mamlaka inatambua umuhimu wa tindikali kwa ajili ya wajasiriamali na marufuku pekee yake isingekuwa na maana, badala yake imeweka utaratibu utakaowezesha udhibiti.
“Pia elimu juu ya matumizi ya tindikali imesaidia. Mpango huu ni endelevu. Sheria inakuja itakayosaidia kuwepo kwa matumizi sahihi ya kemikali na ukaguzi wa vyakula na dawa,” alisema.

Post a Comment

 
Top