0

Allan Goshashi  

iku zote historia hukumbuka mabingwa. Bingwa ni bora kuliko aliyeshindwa. Unaweza kusema mambo mengi kuhusu bingwa, lakini bingwa anapopatikana ni kielelezo cha mafanikio.
Unaweza kusema bingwa siyo kila kitu, sawa, kwa sababu watu wengine huamini wakishiriki na kumaliza mashindano fulani bila matatizo wao ni mabingwa.
Wapo wanaosema bingwa siyo kila kitu ila nia au dhamira ya kutaka kuwa bingwa ndiyo jambo muhimu, wengine husema uzuri wa mchezo kwanza halafu ndiyo bingwa, kwa hiyo ipo mitazamo mingi kuhusu bingwa.
Zipo pia tafsiri nyingi za bingwa, lakini mimi nazungumzia bingwa katika michezo kwa sababu kwa muda mwingi wanamichezo wa Tanzania wameshindwa kuwa mabingwa katika mashindano ya kimataifa.
Kwa mtazamo wangu bingwa huandaliwa, kipaji peke yake hakiwezi kumsaidia mwanamichezo au timu kuwa bingwa, lazima kuwe na maandalizi ya kumuandaa bingwa.
Ninasema hivyo kwa sababu mwanamichezo ili awe bingwa anatakiwa kuandaliwa zaidi katika maeneo matatu ambayo ni nguvu, akili na saikolojia.
Kama wewe ni mfuatiliaji mzuri wa michezo na unayefahamu vizuri maeneo hayo matatu ni dhahiri ukiona timu mbili zinashindana utagundua ni timu gani ina nafasi nzuri ya kushinda kwa sababu unaweza kuona nguvu, akili (kwa sababu ya mbinu zinazotumiwa) au utaona umakini unaotokana na mwanamichezo kujengwa kisaikolojia.
Unaweza kujiuliza kwa nini nguvu?, ni kwa sababu karibu katika kila mchezo mwanamichezo mwenye nguvu inayotakiwa ana asilimia kubwa ya kufanya vizuri katika mchezo husika. Mwanamichezo ni lazima awe na nguvu, kasi na stamina, hivyo vyote hupatikana katika mwili wa mwanamichezo aliyeandaliwa kuwa na nguvu nzuri jambo ambalo haliwezi kufanyika kwa muda mfupi.
Pia unaweza kujiuliza kwa nini akili?, ni kwa sababu mwanamichezo anatakiwa kuwa na maarifa mazuri ya mchezo anaoucheza na kujua sheria zake.
Akili uhitajika kwa mwanamichezo kwa sababu michezo mingi inahitaji mbinu, kwa kuwa zipo mbinu za kushambulia na kuzuia, kwa mfano katika mchezo wa kikapu mchezaji anatakiwa kujua mbinu za kufunga na kupata pointi, lakini anatakiwa pia kufahamu mbinu za kuzuia mpira, kutoa pasi sahihi, kuiba mpira au kuingilia pasi za timu pinzani.
Vilevile akili uhitajika kwa wanamichezo kwa sababu makocha wanakuwa na mikakati yao ya kutaka kuisaidia timu kushinda mechi hivyo lazima wachezaji wamuelewe mwalimu, kwa mfano wapo makocha ambao huwafundisha wachezaji wao kutumia macho kudanganya wanamichezo wa timu pinzani wanapokuwa uwanjani na mkakati huo umefanikiwa sana kwa makocha katika mchezo wa soka au kikapu.
Unaweza pia ukajiuliza kwa nini saikolojia?, ni kwa sababu wanamichezo walioandaliwa vizuri kisaikolojia wana uwezo wa kuifunga timu nzuri yenye wachezaji wenye vipaji kama hawajaandaliwa vizuri kisaikolojia.
Makocha nao huwa wanawapa maneno mazuri wachezaji wao ili kuwafanya wapambane kwa uwezo wao wa juu, ambapo hali hiyo uhitaji mchezaji aliyeandaliwa kisaikolojia kumuelewa kocha wake akiwa mchezoni.
Ipo mifano mingi katika masuala ya nguvu, akili na saikolojia kwa wachezaji ambayo wachezaji wanaweza kuipata kama wakiandaliwa vizuri kwa muda mrefu.
Mambo yote hayo yanataka viongozi wa michezo wanaofahamu masuala ya michezo na wenye elimu ya biashara, pia michezo inatakiwa kuongozwa na watu wenye uzoefu wa programu, utawala hasa katika bajeti, kupanga matukio na masuala ya masoko.
Lazima tuelewe hivi sasa michezo inahitaji wanamichezo weledi kwa hiyo mahitaji ya viongozi weledi pia ni makubwa.
Kinachoonekana nchini ni kwamba hatuna viongozi weledi wa michezo nchini watakaowezesha kuhakikisha mabingwa wanaandaliwa nchini ila tunategemea tu vipaji vya wachezaji kutafuta ubingwa katika mashindano mbalimbali na hata matokeo tunayoyapata kimataifa yanaonyesha hivyo.

Post a Comment

 
Top