0
Masasi. Rais Jakaya Kikwete amezindua mradi wa maji wa Mbwinji unaotoa huduma kwa wakazi wilayani hapa na Nachingwea mkoani Lindi na kulifanya tatizo hilo sugu la ukosefu wa maji lililokuwa linawakabili wakazi wa wilaya hizo kuwa historia.
Akizindua mradi huo juzi, Rais Kikwete alisema ni faraja kwake kuweka historia katika tatizo la maji kwenye wilaya hizo kutokana na yeye mwenyewe kuwa miongoni mwa wananchi walioonja adha hiyo. “Niliwahi kuishi Nachingwea wakati huo nilikuwa katibu wa CCM wa wilaya kabla sijahamia Masasi. Mimi ni miongoni mwa walionja adha hii ya kukosa maji, hivyo niliahidi wakati wa kampeni zangu kuwa nitahakikisha tatizo la maji Masasi na Nachingwea linakuwa historia na sasa imewezekana,” alisema Kikwete akionekana mwenye furaha
Aliongeza kusema: “Kazi kubwa iliyopo ni kuilinda miundombinu hii isihujumiwe, itunzeni ili nanyi iwatunze. Hakikisheni maeneo ya vyanzo vya maji kule Mbwinji hayaharibiwi, sheria zipo na ikibidi basi tangazeni kwenye gazeti la Serikali kuwa ni eneo la hifadhi.”
Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira wa Masasi-Nachingwea (Manawasa), Nuntufye Mwamsojo alimwambia Rais katika taarifa yake kuwa ujenzi wa mradi huo ulianza Februari 2011 na kuligharimu taifa Sh31 bilioni.
Alibainisha kuwa mradi huo utanufaisha wakazi 102,696 wa Mji wa Masasi na kwa sasa wakazi 83,128 (sawa ana asilimia 81) wamefikiwa na huduma hiyo, wakati katika Mji wa Nachingwea wakazi 77,207 (sawa na asilimia 64) wamefikiwa na huduma hiyo.
Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe alimpongeza Rais kwa kuwekeza nguvu zake katika mradi huo na kumwomba jitihada kama hizo zifanywe katika miradi mingine pia. “Mheshimiwa Rais katika bajeti ya mwaka jana nilipangiwa Sh600 bilioni hadi mwaka unaisha nilipewa Sh140 bilioni tu. Hii ndiyo sababu miradi mingi ya maji imekwama,” alisema Maghembe.

Post a Comment

 
Top