0
Dar es Salaam. Sekta ya kilimo nchini itakua kwa kasi endapo msaada wa magari kwa taasisi zinazosimamia sekta hiyo utatumika ipasavyo kuwawezesha watendaji kuzungukia maeneo mbalimbali kufanya utafiti.
Umoja wa Ulaya (EU) umetoa magari 21 ili kusaidia sekta ya kilimo nchini, ambayo hutegemewa na Watanzani wengi.
Akizungumza wakati wa kukabidhi magari hayo, kiongozi wa ujumbe wa EU, Tom Vens alisema wanafanya jitihada za kubadilisha sekta ya kilimo barani Afrika ili ibadilishe maisha ya watu wake.
Vens alisema mabadiliko yatafanyika kama taasisi za kitafiti zitawezeshwa vitendea kazi muhimu, baadaye taasisi hizo kuwafikia wananchi moja kwa moja na kuwapa ushauri wa kitaalam.
Alisema ushirikiano kati ya EU na Tanzania umebainisha usalama wa chakula kama kipaumbele katika uhusiano wao. Mazao yanayolengwa zaidi ni kahawa, pamba, chai, uvuvi na mazao ya mbogamboga.
“Taarifa sahihi, mtaji na ujuzi ndiyo vitu muhimu katika kukuza kilimo. Pato la taifa litokanalo na kilimo litaongezeka na kulinufaisha taifa,” alisema Vens.
Baada ya kupokea msaada huo, katibu mkuu wa Wizara ya Fedha, Dk Servacius Likwelile alisema magari hayo yatagawiwa kwa taasisi za kitafiti zilizo chini ya Wizara ya Kilimo na Chakula.
Taasisi hizo ni ya Utafiti wa Kahawa (TCRI), Bodi ya Pamba (TCB), Maabara ya Mazao ya Uvuvi (NFCL), Shirika la Viwango (TBS) na Taasisi ya Chai (TIT). Magari hayo yana thamani ya Sh8 bilioni.

Post a Comment

 
Top