0

Waziri wa Fedha Saada Mkuya.PHOTO|FILE 

Kwa ufupi
Tukipitia bajeti hizo na ya mwaka ujao wa fedha, tunagundua kwamba kinachofanywa na watayarishaji wa bajeti hizo ni kubadilisha tu takwimu za mwaka hadi mwaka na kuishia na bajeti zinazotegemea mapato yatokanayo na pombe, sigara na soda.

Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka ujao wa fedha ilipitishwa bungeni juzi baada ya wabunge kuijadili kwa siku saba. Kama wananchi wengi walivyoshuhudia, Bajeti hiyo iliibua mijadala mikali, huku wabunge wengi wakitishia kutoiunga mkono kutokana na Serikali kushindwa kubuni vyanzo vipya vya mapato, huku misamaha ya kodi ikiendelea kuikosesha fedha nyingi na kusababisha nakisi kubwa katika Bajeti hiyo.
Haishangazi hata kidogo kuona kwamba Bajeti hiyo ilipitishwa kwa idadi kubwa ya ‘kura za ndiyo’ 234, huku wabunge 66 wa vyama vya upinzani waliopiga kura wakiikataa. Kinachoshangaza ni pale wabunge wengi wa chama tawala waliokuwa wametishia kuikwamisha waliipitisha kwa misingi ya kiitikadi na msukumo wa kile kinachotajwa kuwa ni kutunza nidhamu ya chama. Hivyo, pamoja na upungufu mkubwa uliomo, wabunge hao waliona bora kufunika kombe ili mwanaharamu apite.
Majumuisho ya Waziri wa Fedha, Saada Salum Mkuya kuhusu mapendekezo ya wabunge waliochangia mjadala wa Bajeti hiyo hayakuonyesha kama Serikali imeyapa mapendekezo ya wabunge uzito wa kutosha, isipokuwa katika maeneo machache kama misamaha ya kodi. Serikali ililiomba Bunge liidhinishe jumla ya Sh19.9 trilioni kwa matumizi ya kawaida na miradi ya maendeleo. Lakini katika kuthibitisha kwamba bajeti hiyo siyo endelevu, fedha za maendeleo zilizokuwa zimetengwa ni Sh6.44 trilioni sawa na asilimia 32.4 tu ya bajeti, huku fedha zilizoombwa kwa matumizi ya kawaida ni Sh13.4 trilioni sawa na asilimia 67.4 ya bajeti hiyo.
Wabunge walitaka kipaumbele kiwekwe kwenye sekta za elimu, afya, maji, miundombinu na nyingine kadhaa zilizoainishwa katika mpango wa Serikali wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN), badala ya fedha nyingi kutengwa kwa ajili ya matumizi yasiyo muhimu kama semina, safari za viongozi, posho, magari ya kifahari na matumizi mengine ya anasa. Kwa mfano, safari za Rais zilitengewa Sh50 bilioni, wakati Kilimo kilitengewa Sh51 bilioni. Hata hivyo, pamoja na Kamati ya Bunge ya Bajeti kuibana Serikali, ni Sh165.8 bilioni tu zilizopunguzwa kwenye matumizi yasiyo na tija kwa taifa.
Katika majumuisho ya Waziri Mkuya, jambo lililojitokeza bayana ni kwamba Serikali haijawa tayari kubadilika na kutumia ubunifu katika kutayarisha bajeti za Serikali, badala ya kuendelea na bajeti za mazoea. Katika utayarishaji wa Bajeti, lazima Wizara ya Fedha iwahusishe wadau, kama Repoa, Twaweza, TGNP na ESAURP ili ichote fikra mpya na kuleta mabadiliko yanayoweza kuliwezesha taifa kuondokana na Bajeti tegemezi. Tumekuwa tukisema bajeti za Serikali zinarudufiwa, kwa maana ya kubeba maneno, maelezo na maudhui yanayofanana sana na ya bajeti za miaka iliyopita. Tukipitia bajeti hizo na ya mwaka ujao wa fedha, tunagundua kwamba kinachofanywa na watayarishaji wa bajeti hizo ni kubadilisha tu takwimu za mwaka hadi mwaka na kuishia na bajeti zinazotegemea mapato yatokanayo na pombe, sigara na soda.
Inasikitisha kuona kwamba Waziri Mkuya hakutoa sababu za Serikali kushindwa kutekeleza mapendekezo ya Kamati ya Bunge ya Bajeti kuhusu vyanzo vipya vya mapato, ambavyo vingemaliza tatizo la nakisi katika bajeti za Serikali kama mapendekezo hayo yangetekelezwa. Pamoja na kusema Serikali inahitaji muda zaidi kufanya utafiti wa kuona utekelezaji wa mapendekezo hayo, hakusema hatua ambazo Serikali imechukua hadi sasa kutokana na wabunge kupigia kelele suala hilo mwaka hadi mwaka.

Post a Comment

 
Top