0
Juni 18 mwaka huu, Bodi ya Pamba (TCB) ilitangaza kuanza kwa msimu mpya wa uvunaji wa zao hilo, sambamba na kutangaza bei mpya kwa msimu wa mwaka 2014/15 kwa wakulima kutoka Kanda ya Ziwa.
Uzinduzi huo ulifanyika kwenye Kijiji cha Isole, Wilaya ya Sengerema na kuhudhuriwa na wakulima ambao walikuwa na shauku ya kutaka kujua wanafaidika na nini mwaka huu baada ya kulima pamba?
Nikiwa miongoni mwa watu waliohudhria sherehe za kutangazwa kwa bei mpya ya msimu wa pamba, nilishuhudia waziwazi nyuso za wakulima waliohudhuria sherehe hizo zikiwa na matarajio makubwa ya kupata faida kwa msimu huu.
Lakini, baada ya makamu mwenyekiti wa TCB, George Wassira kutangaza bei mpya ya pamba, zilisikika sauti za chinichini kutoka kwa wakulima ambazo ziliashiria kutoridhishwa na bei hiyo.
Makamu huyo mwenyekiti wa TCB alitangaza kuwa kwa msimu wa mwaka 2014/2015 pamba imeongezeka kwa Sh50, kutoka Sh700 kwa kilo moja kwa msimu wa mwaka 2013/2004 hadi kufikia Sh750 kwa kilo kwa msimu wa mwaka 2014/15.
Miongoni mwa malalamiko ya wakulima ni pamoja na gharama kubwa wanazotumia wakati wa kuandaa mashamba na kwamba na bei iliyotangazwa na TCB kuwa ndogo, haiwezi kufikia hata robo ya gharama wanazotumia.
Kila msimu wa kuvuna pamba unapokaribia kumekuwa na malalamiko mengi kutoka kwa wakulima wa zao hilo, hivyo kuna haja kwa Serikali kutafuta njia mbadala ya kuwasaidia wakulima hawa ili waweze kupata faida.
Hata hivyo, moja ya vitu ambavyo wamekuwa wakilalamikia wakulima hao ni hatua mbalimbali ya upangaji wa bei. Mosi wanadai kuwa hawashirikishi, hivyo kama suala hili ni vyema likatafutiwa ufumbuzi ili kuwafuta machozi wakulima hawa ambao kila kukicha wanakuwa na malalamiko lukuki.
Pili, wakulima wamekuwa wakidai Bodi ya Pamba ndiyo wapangaji wa bei na hao ndiyo wanunuzi wa pamba, hivyo ni wazi haiwezi kutoa bei zenye faida kwao. Kama jambo hilo ni kweli ni vyema Serikali ikalitazama na kuchukua hatua stahiki. Siyo vyema kuona mtu ambaye anategemea kilimo kama sehemu ya maisha yake, kupata hasara na kuwanufaisha watu wachache.
Hayo ni baadhi ya malalamiko, ukiondoa mengine ya utumiaji wa mizani ya digiti ambazo wakulima wengi wanadai kwamba zinawaibia zaidi kwa kuwa hawafahamu jinsi ya kuzitumia.
Si jambo la busara kama hujatoa elimu sahihi ya matumizi ya kitu halafu unawapelekea wakulima watumie wakati unafahamu wazi kwamba wengi wao wana elimu ya kawaida.
Baadhi ya maneno ambayo wakulima wa pamba walitamka ni pamoja na “elimu zetu ni za kawaida, leo tunaletewa mizani ya digiti ili kupima pamba zetu. Hii kama siyo njia ya kutunyonya na kutaka kutuibia, ni nini?” alihoji mkulima mmoja.
Ni vyema Serikali kupitia TCB kulitazama jambo hilo kwa kina ili kuhakikisha inaondoa malalamiko ya wakulima na kuwawezesha kupata faida kupitia kilimo chao cha pamba.
Kwa sasa wakulima wengi wa pamba ambao ni wa kawaida wanadai kutumia Sh30,000 kwa kulima na kukodi shamba ni Sh100,000.
Kwenye hatua za mwanzo jambo hili linawasababishia kutumia gharama kubwa tofauti na matarajio yao wakati bei zinapotangazwa.
Aidan Mhando ni mwandishi wa habari wa gazeti la Mwananchi.

Post a Comment

 
Top