0
Rufiji ni wilaya tajiri sana. Sidhani kama wananchi na viongozi wanalielewa hilo. Kuwa mto mkubwa kuliko yote nchini, unapita wilayani hapo na kuachia tani za maji baharini na kutapanya mbolea asili huko na huko ardhini. Ni utajiri ambao unahitaji watu wenye kufikiri kwa makini, na wanaotaka maendeleo ya wananchi wao. Na kuwa Rufiji inaweza pia kuwa sehemu ya utalii wa wanyama kama viongozi na wananchi wangekubali hilo. Nilikuwa Rufiji Delta hivi karibuni. Awali sikuwa nina picha kamili ya delta hiyo ikoje. Na kwa kweli siwezi kuielezea ikoje kwani ninachoweza kusema tu ni kuwa mto Rufiji umezaa mito mikubwa, baadhi ikiwa na upana wa nusu kilomita ikitengeneza visiwa vingi ambako watu wanaishi.
Na kuwa hata utumie mtumbwi wenye injini, huwezi ukatembelea kila mahali kwa siku moja. Unahitaji siku mbili. Delta hii ina utajiri mwingi.
Kwanza ni utajiri wa maji ambayo ndani yake unaweza kufanya uvuvi wa samaki na uvuvi wa dagaa. Katika pitapita yangu na mtumbwi katika delta hiyo tuliona uwezekano wa kuwekeza katika uvuvi. Wavuvi walioko ni wale wa kutumia mitumbwi ya makasia, ambayo huwezi kutegemea kuwa na tija kubwa.
Lakini tukakutana na wavuvi wawili wa samaki aina ya kamba ambao mtumbwi wao ulijaa samaki hao wakiwa hai, sijui walikuwa wakienda nao wapi? Tulipowauliza bei walisema kuwa ni Sh1,000 kwa fungu la kupima kwa mkono.
Nilinunua fungu tatu,na wenzangu wakanunua mengi zaidi, ni kama kilo sita kwa jumla;, kwa ukubwa wa Kamba wale, tena wakiwa hai, hotelini tungenunua kama kwa Sh50,000. Nina uhakika kabisa kwa kuwa na uratibu mzuri sana wa kimazingira, na wa kibiashara, wavuvi wale wanaweza kupata faida kubwa kwa biashara hii ya Kamba. Lakini sijui kama viongozi wanajua kama huu ni utajiri mkubwa sana. Ukiachia mbali hilo, kuna utajiri wa samaki wa kawaida ndani ya mito mingi inayopishana eneo hili.
Delta hiyo ina utajiri wa kihistoria! Hapo ndipo palipojengwa boma la kwanza, mwaka 1906 la Mjerumani kabla ya lile la Utete. Boma hilo liko hadi leo, likitumika kama zahanati ya kata ya Salali.
Na jirani na hapo, kama mita miambili ndipo ilipo meli ya kivita ya Kijerumani ya Konisberg ambayo ilipigwa mabomu na majeshi ya Waingereza.
Ndiyo niliyoilalamikia katika makala iliyopita; na kuwa hapo vita vilipiganwa sana kwa vile sio tu koloni la mjerumani lilikuwa likitetea, bali pia kulikuwa na ofisi ya serikali ya kikoloni. Lakini utajiri huu wa kihistoria, kama nilivyosema, umetelekezwa na kuachwa wawindaji wa skrepa waivamie na kuimaliza kwa kuikatakata.
Kabla ya watu kuongezeka eneo hilo, lilikuwa sehemu ya hifadhi ya wanyama ya Selous.
Na si miaka mingi iliyopita tembo, simba na wanyama wengine walikuwa wakionekana katika msitu unaopakana na delta hii. Msitu huu uko chini ya hifadhi.
Kumbe kama serikali ya Wilaya ya Rufiji ingeamua, ingeweza kuufanya msitu huu kuwa zoo (hifadhi ya kutembelea wanyama kwa burudani), au mbuga kamili ya wanyama , ambayo ingefanya tuwe na mbuga ya pili nchini inayopakana na Bahari ya Hindi baada ya Saadani.
Inanishangaza kuwa tunataka kuwa na utalii wa ndani, lakini kivutio kama hiki cha Rufiji Delta kinapuuzwa. Delta hii ingeweza kuvutia watalii wa kimazingira (eco-tourists), ambao wangetaka kupata burudani ndani ya mito hii mikubwa ya delta, na kutembelea hifadhi ya mikoko na kujua maisha ya watu.Kwa kuwa na kambi za muda kwenye eneo hilo, ingeweza kuwafanya watalii kufika na kutoka, na hivyo kuongezea wananchi kipato kutokana na utalii. Badala yake, tunaruhusu wananchi kufanya kilimo ambacho kinaharibu uoto na mifumo mingine ya bionuwai. Rufiji iamke usingizini.

Post a Comment

 
Top