0



Posted  Alhamisi,Juni26  2014  saa 14:42 PM
Kwa ufupi
Mjasiriamali anatakiwa kuwa na uelewa wa biashara anayoifanya kwani uelewa au weledi wa jambo ni kivuko kimojawapo kati ya vivuko vingi ambavyo humvusha mwanadamu kutoka katika hali duni kwenda katika hali nzuri.

Wataalamu mbalimbali wa uchumi duniani wamefanya utafiti na kubaini kuwa biashara zinazoanza zinakabiliana na changamoto mbalimbali kwani takriban asilimia 64 ya biashara hushindwa kuendelea ndani ya miaka mitano tangu zimeanzishwa. Hii ina maana kuwa kiasi cha biashara zinazokua ni kidogo sana ukilinganisha na kile kinachoishia njiani.
Kufa kwa biashara nyingi zinazoanza ndani ya miaka mitano kunatokana na sababu mbalimbali hasa zinazohusu mjasiriamali mwenyewe.
Sababu nyingine ni mazingira, mfumo mzima wa nchi katika uandaaji wa mazingira mazuri ya kukuza biashara na matatizo ya asili ambayo yanakuwa nje ya uwezo wa mwanadamu katika kukabiliana nayo.
Kwa vile lengo la kufanya biashara ni kutaka kuona kuwa biashara husika inakua na kuwa kampuni kama biashara husika haikuanzishwa kama kampuni, zifuatazo ni mbinu zinazoweza kutumiwa na mjasiriamali katika kuhakikisha biashara anayoianzisha haiishii njiani, bali inapiga mbizi ndani ya mawingu makubwa na ngurumo za radi kuelekea kwenye sehemu salama na yenye mafanikio.
Mjasiriamali anatakiwa kufanya tathmini ya kina juu ya biashara yake ili aweze kubaini fursa na changamoto zilizoko kwa lengo la kuepukana na anguko analoweza kulipata katika safari ya biashara yake.
Ikumbukwe kuwa, wakati mwingine mjasirimali huamua kufanya biashara bila kufanya tathmini ya kina kwa kuwa tu ana mapenzi na biashara hiyo na matokeo yake huwa ni anguko la kibiashara kwani kuwa na mapenzi ya kitu fulani huweza kuwa na upofu ambao madhara yake ni makubwa kibiashara.
Mjasiriamali anatakiwa kuwa na uelewa wa biashara anayoifanya kwani uelewa au weledi wa jambo ni kivuko kimojawapo kati ya vivuko vingi ambavyo humvusha mwanadamu kutoka katika hali duni kwenda katika hali nzuri.
Mara nyingi wajasiriamali wengi huishia njiani kutokana na uelewa mdogo wa biashara anayoifanya ambao husababisha ashindwe kukabiliana na changamoto za wakati na mazingira.
Mjasiriamali anatakiwa kuwa na ufshsmu wa mahitaji ya kitaalamu ya biashara yake ili kuepukana na changamoto zinazoweza kuangusha biashara yake, kwa mfano, kama wewe ni mfanyabiashara wa magari unatakiwa uwe unajua angalau nusu ya kila jambo linalohusiana na magari.
Mjasiriamali anatakiwa kuwa na uelewa juu ya masuala ya kifedha kama vile kutunza kumbukumbu za mauzo na manunuzi ikiwa ni pamoja na mambo mengine ya kifedha yanayohusiana na biashara yake.
Tafiti zinaonyesha kutokuwa na uelewa wa masuala ya kifedha ni moja ya sababu za kushindwa kukua kwa baadhi ya biashara duniani kote.
Mjasiriamali anatakiwa kuwa na uelewa juu ya sheria zinazohusiana na biashara anayoifanya ili kuepukana na kero ndogondogo zinazoweza kuangusha biashara yake kwani uzoefu unaonesha kuwa baadhi ya sehemu hapa nchini zimekuwa na baadhi ya watendaji wa Serikali ambao huwa na malengo ya kuwakomoa wajasiriamali kwa kutoa vitisho kwa baadhi ya wajasiriamali ambao kwa kutoelewa sheria ndogondogo, huamua kutelekeza biashara zao.
Ikumbukwe kuwa kuna wataalamu waliobobea katika masuala ya biashara kama vile sheria, uongozi na usimamizi wa biashara ambao kazi yao ni kushauri namna ya kufanya biashara kwa mafanikio kwani kazi ya mjasiriamali inafanana na msemo wa Kichina usemao “kikombe kilichojaa, hakina manufaa” kwa maana kuwa mjasirimali hajabobea katika kila jambo la biashara anayoifanya bali mwenye uelewa wa jumla wa biashara anayoifanya.
Mwandishi wa makala haya ni mtaalamu wa ujasiriamali na mtunzi wa vitabu

Post a Comment

 
Top