0
Dar es Salaam. Visima vingi vya maji vilivyochimbwa jijini Dar es Salaam na unga wa lishe kwa watoto umeelezwa kutokuwa salama kwa afya za watumiaji, kulingana na utafiti uliofanywa hivi karibuni na Ofisi ya Wakala wa Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA).
Akizungumza wakati wa kuwatembeza katika maabara za mkemia mkuu baada ya uzinduzi wa bodi ya wakurugenzi wa wakala huyo jijini Dar es Salaam jana, Mkemia Mkuu wa Serikali, Profesa Samwel Manyele alisema sampuli zilizochukuliwa hivi karibuni zimebainisha.
Alisema maji yalichukuliwa kutoka katika visima tofauti na kufanyiwa utafiti na maabara ya wakala huyo na kubainika kuwa mengi si salama kwa matumizi ya binadamu na utafiti zaidi unaendelea ili kubaini athari zaidi ambazo zinaweza kusababishwa na maji hayo.
“Tumechukua sampuli chache na zimeonyesha kuwa maji hayo siyo salama hata kidogo na tunaendelea na utafiti kujua athari zaidi ambazo zinasababishwa na maji hayo” alisema.
Alisema hali kama hiyo imeonekana pia katika unga wa lishe ambao unauzwa mitaani.
Alisema hali siyo nzuri kwa chakula hicho cha watoto ambacho kimekuwa kikitumiwa na watu wengi nchini miaka ya karibuni na walifanya uchunguzi huo wa kimaabara ikiwa ni sehemu ya mipango ya ofisi hiyo ya mkemia kuchukua sampuli za vyakula tofauti na bidhaa zingine kwa aili ya utafiti.
Profesa Manyele alisema wanatarajia kuwasilisha bungeni mapendekezo ya muswada wa mabadiliko ya sheria ambayo yatatoa mamlaka kwa wakala wa mkemia mkuu wa serikali kuchukua sampuli ya vyakula, dawa au bidhaa zingine zozote na kuzifanyia uchunguzi katika maabara na kutoa mapendekezo serikalini.

Post a Comment

 
Top