0
Kuwa na makazi ni moja ya mahitaji muhimu ya binadamu, kwa kutambua hilo Serikali imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali kuwawezesha watumishi wake na wananchi kwa jumla kupitia mashirika mbalimbali, waweze kumiliki nyumba hata kwa njia ya mkopo.
Kumekuwa na miradi mingi ya ujenzi wa nyumba mbalimbali zikiwamo za ofisi na makazi, ikitekelezwa chini ya Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSPF), Mfuko wa Pensheni kwa Mashirika ya Umma (PPF) na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA).
Mingine ni Mfuko wa Akiba kwa Watumishi wa Serikali (GEPF) na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi za Jamii (NSSF) pamoja na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).
Miezi minne iliyopita Serikali imeanzisha kampuni maalumu iitwayo Watumishi Housing Ltd (WHC), ambayo imepewa jukumu la kusimamia mpango mahususi wa kujenga nyumba 50,000 ambazo itawakopesha kwa masharti nafuu watumishi wa umma, ikiwa na lengo la kuwajengea maisha bora.
Ofisa Mtendaji Mkuu wa WHC, Dk Fred Msemwa anazungumzia hatua hiyo ya Serikali, akisema kuwa mpango huo unaanza kutekelezwa mwezi Juni mwaka huu mkoani Dodoma katika eneo la Njedengwa.
“Serikali inatambua uhusiano wa karibu kati ya kuwa na makazi bora kuwa na afya, kupata fursa za kiuchumi ikiwamo mikopo, hivyo WHC inajisikia fahari kutimiza ndoto ya watumishi wa umma kuwawezesha kumiliki makazi,” anasema Dk Msemwa.
Anafafanua kwamba WHC inajenga na kuuza nyumba za aina mbalimbali kwa lengo la kukidhi mahitaji na matarajio ya wateja, kulingana na mahitaji kwa kuwa zipo nyumba za chumba kimoja, viwili na vyumba vitatu.
Dk Msemwa anassema pia zipo nyumba zilizoungana au (semi-detached), zilizo pekee (detached) na zile za ghorofa, ambazo zote zinazojengwa kwa kuzingatia utamaduni wa Mtanzania na maendeleo katika mtindo wa maisha ya vijana.
Anabainisha kwamba pia mpango huu wa kuwezesha wananchi kumiliki nyumba umeanza na watumishi wa umma na baadaye utahusisha wananchi wote kwa mkopo ambao unatofauti na aina hii iliyopo katika soko, kwani mingi inaishia miaka 10-15 na michache sana inafika miaka 20.
“Kampuni imepewa jukumu la kuwa mtekelezaji mkuu wa Mpango wa Taifa wa Makazi kwa Watumishi wa Umma, kwa kuwa imebainika watumishi wengi wa serikali, wamekuwa wakikumbana na vikwazo wanapojitokeza kwenda kuomba kukopeshwa nyumba, kutokana na kushindwa kumudu masharti yaaliyowekwa,” anasema.

Post a Comment

 
Top