Urasimishaji biashara, yaani kuifanya
biashara itambulike kisheria, ni hatua muhimu sana katika maendeleo ya
biashara na taifa kwa ujumla, ingawa wajasiriamali wengi hawajarasimisha
biashara zao kwa kuwa baadhi yao hawajua hatua mbalimbali zinazotakiwa
kufuatwa.
Kitendo cha wajasiriamali hao kutojua namna ya
kurasimisha biashara zao kinaashiria mambo mengi ikiwa ni pamoja na
kasoro za mfumo wetu wa elimu ya msingi hadi vyuoni katika kuwaandaa
vijana kwa ajili ya maisha ya baadaye nje ya mfumo wa kuajiriwa, na
kushindwa kwa mamlaka husika katika kutoa elimu na vishawishi kwa
wajasiriamali juu ya urasimishaji wa biashara zao.
Kabla ya kuanza kuelezea hatua hizo hatuna budi
kukiri kuwa kila mfanyabiashara huwa na malengo yake kibiashara na hatua
anazochukua mara nyingi huwa zinaendana na malengo yake kibiashara.
Haiyumkiniki kuwa na wajasiriamali ambao
wangependa biashara zao ziwe na majina yanayotambulika kisheria kama
vile “Hope Publishers” na kuna baadhi yao wangependa biashara zao ziwe
na majina yao waliyopewa na wazazi wao kama vile “Masawe Kinabo,”
yasiyotambulika kama majina ya biashara kisheria.
Kwa mjasiriamali ambaye angependa kuwa na jina la
biashara ambalo linatambulika na kulindwa na sheria ya nchi, anatakiwa
kuanzia BRELA au katika ofisi za mabaraza/mamlaka za biashara zilizo
karibu na mhusika ambako atapewa fomu maalumu na kuijaza na wao
kuiwasilisha BRELA.
Ili kuhakikisha kuwa jina la biashara halifanani
na majina mengine ambayo yameshatumika sharti lifanyiwe uchunguzi ama
kwa mjasiriamali mwenyewe kupitia tovuti ya BRELA na kisha kupeleka
BRELA kwa ajili ya uthibitisho ama kupeleka moja kwa moja BRELA ambapo
hufanyiwa uchunguzi na kwa kawaida zoezi hili ambalo hugharimu kiasi cha
shilingi 6,000/= hukamilika ndani ya siku saba au zaidi kulingana na
hali halisi ya utendaji kazi pamoja na matatizo mengine yenye kuhusiana
na mwombaji.
Baada ya kupata cheti cha jina la biashara,
mjasiriamali anatakiwa kwenda Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa ajili
ya kuomba namba ya mlipa kodi (TIN), ambapo hupewa fomu mbili za
kujaza; fomu maalumu ya TRA kwa ajili ya kuijaza yeye mwenyewe na barua
ambayo inatakiwa kujazwa na mwenyekiti wa mtaa kama uthibitisho wa
kufanya biashara katika eneo husika. Kwa wale ambao wanaona biashara yao
haihitaji kuwa na jina la biashara kutoka BRELA, wanaenda moja kwa moja
Mamlaka ya Mapato Tanzania ambako hupewa fomu mbili; fomu maalumu ya
TRA kwa ajili ya kujazwa na mhusika mwenyewe na barua ambayo hujazwa na
mwenyekiti wa mtaa kama uthibitisho wa kufanya biashara katika eneo
husika, na urejeshaji wa fomu hizo huambatana na mkataba wa upangaji wa
mahali anapofanyia biashara.
Kama mjasiriamali tayari ana namba ya mlipa kodi
ya leseni ya gari/udereva, anatakiwa kujaza namba hiyo kwenye fomu
husika akiambatanisha na cheti/leseni kivuli cha namba husika na
kupeleka TRA kwa ajili ya uthibitisho na kuipa matumizi mengine ya
biashara binafsi.
Baada ya kupata namba ya mlipa kodi, mjasiriamali
anatakiwa kwenda mamlaka za halmashauri za wilaya/mji/manispaa/jiji kwa
ajili ya kuomba leseni ya biashara akiwa na kivuli cha cheti cha mlipa
kodi kutoka mamlaka ya mapato ya TRA, mkataba wa upangaji wa mahali
anapofanyia biashara na nakala mojawapo ya kivuli cha kitambulisho cha
uraia/kupigia kura au udereva, ambapo atapewa fomu ya kujaza yenye
maelezo ya aina za biashara na masharti ya kupata leseni, na baada ya
hapo maofisa biashara wa mamlaka husika hujiridhisha na kutoa leseni.
Mwandishi wa makala ni mtaalamu wa ujasiriamali.
Post a Comment