0
Siku hizi ukipita mitaani katika mikoa mbalimbali si jambo la ajabu kusikia na kusoma matangazo yanayoelekeza mahali fedha chakavu zinaponunuliwa.
Tangazo moja linalotoka katika kipaza sauti kilichopo stendi ya mabasi ya daladala ya Mbagala Rangi Tatu, wilayani Temeke linasema: “Tunauza dawa ya kuua panya, inzi na mende, pia tunanunua hela mbovu, mia tano, elfu moja na dola, tunanunua”.
Ingawa tangazo hilo linataja bidhaa aina tofauti, linanivutia kusogea karibu na kuzungumza na mnunuzi wa fedha hizo, John Kiduko anayesema watu wengi wana fedha zilizochakaa, wanaziweka nyumbani wakidhani thamani yake imekwisha.
Anaeleza kuwa tangu aanze kununua fedha chakavu watu wengi wamejitokeza na kushukuru kuwa kumbe kuna watu wanaonunua fedha zilizochakaa.
Huku akiamini mimi ni mmoja wa wateja wake, anavuta droo yenye fedha alizozinunua na kunionyesha, kisha anatoa maelezo ya namna kila moja ilivyochakaa.
“Hela zenyewe ziko hivi, nyingine bado mpya kabisa lakini zimechanika,” anasema.
Mfanyabiashara mwingine, Victor Asenga anasema kwa siku ananunua noti za Sh500 nyingi zaidi ikilinganishwa na aina nyingine za fedha.
Ananionyesha fedha alizonunua, na nabaini kuwa pamoja na kuchakaa pia zipo ambazo zimepakwa rangi, mafuta na nyingine zikiwa na mabaki ya damu.
“Tunanunua hela mbovu kama hizi (ananionyesha Sh500 iliyochakaa lakini haijachanika). Sharti letu sisi tunanunua noti ambayo bado namba zake zinaonekana, kama imefutika sana basi hiyo haitufai,” anasema.
Ninapomuuliza kwa nini noti za Sh500 zilizochakaa ndiyo nyingi zaidi, anasema: “Sina jibu kamili, nadhani ndizo zilizo nyingi mikononi mwa watu, kama siyo hivyo basi kutakuwa na sababu nyingine.”
Mtandao wa biashara
Naye, Elia Lyimo anayefanya biashara hiyo na ya kuuza chenji kwa makondakta wa daladala, anasema kazi hiyo wamepewa na mtu anayemtambulisha kwa jina la ‘bosi’ wao ambaye hupita kila baada ya wiki moja kukusanya fedha hizo na kuzipeleka Benki Kuu ya Tanzania (BoT).
“Kuna jamaa mmoja anayefanya kazi Benki Kuu ndiye aliyetupa kazi ya kununua fedha mbovu, huwa anakuja kuzikusanya na kuondoka nazo,” anasema Lyimo.
Waziri alonga
Waziri wa Fedha na Uchumi, Saada Mkuya anasema kuwa wafanyabiashara kupita mitaani na kukusanya fedha chakavu siyo kosa, tatizo ni kuzinunua noti hizo kwa punguzo la asilimia hamsini.
Pia anasema wafanyabiashara hao siyo mawakala wa Benki Kuu, hivyo anawataka wananchi wenye fedha zilizochakaa kuzipeleka wenyewe benki.
“Ingekuwa busara zaidi kama wananchi wenyewe wakafika Benki Kuu au kwenye benki za biashara kubadilisha hizo fedha. Kimsingi hizo zina thamani sawa na zile zilizochakaa,” anasema.
Tamko la Benki Kuu
Katika taarifa yake kwa gazeti hili, Benki Kuu ya Tanzania (BOT) inasema kuwa huduma ya kubadilisha noti chakavu hutolewa bure na benki hiyo kwa sharti kuwa anayepeleka noti anarudishiwa fedha kwa thamani ile ile.
Mkurugenzi wa huduma za kibenki wa benki hiyo, Emmanuel Boaz anasema hawana madalali wa kununua noti chakavu na kusisitiza kwamba biashara hiyo kimsingi siyo halali.
“Wananchi walio na taarifa za biashara inayoendelea kinyume na utaratibu huo ni vyema wazitaarifu ofisi za Benki Kuu au kuzipeleka kwa vyombo vya dola ili hatua za kisheria zichukuliwe,” anaeleza.
Pia anasema kuwa ubadilishaji wa noti chakavu hufanyika makao makuu Dar es Salaam na katika matawi yake yaliyoko Mwanza, Mbeya, Arusha na Zanzibar.
Sababu za noti kuchakaa
Mfanyabiashara wa muda mrefu katika Soko Kuu la Kariakoo, Uswege Mwambambe anasema moja ya sababu zinazofanya noti nyingi kuchakaa haraka ni pamoja na tabia ya baadhi ya watu kupenda kuzifunga kwenye nguo na kuzishika kwa mikono michafu.
“Nimekuwa nikipokea noti ambazo zimekunjwa vibaya sana, nyingine hazijachanika lakini zimechafuka kwa mafuta au hata damu, hasa zinazotoka buchani kwa wauza nyama,” anasema na kuongeza:
“Baadhi ya watu hawana nidhamu kabisa ya kutunza fedha, fikiria kwamba kila siku unapokea noti moja iliyochorwa au kuchanwa kwenye pembe, kuna noti ngapi za aina hiyo nchi nzima?”
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitivo cha Biashara cha Chuo Kikuu cha Tumaini Dar es Salaam, Deogratius Massawe anasema baadhi ya watumiaji wa dawa za kulevya wanachangia kuharibu noti kwa kuchomoa uzi wa usalama kwa minajili ya kwenda kuutumia katika uvutaji wa unga.
“Mateja huchomoa ule uzi unaowekwa kwenye noti na kuuchanganya na vitu vingine kwa ajili ya kuvutia unga. Hii ni tabia ya muda mrefu na inaharibu sana fedha,” anasema.
Anaongeza kuwa hali hiyo inapaswa kukomeshwa mara moja kwani inaharibu mwelekeo wa kiuchumi wa Taifa.

Post a Comment

 
Top