0
Serikali na taasisi mbalimbali za kilimo zimekuwa zikifanya utafiti wa kilimo na mazao kwa lengo la kuboresha kilimo nchini.
Hata hivyo inaonekana kwamba wakulima hasa wadogo wamekuwa hawashirikishwi kwenye hatua za awali za utafiti na kusababisha kupatikana kwa majibu au taarifa ambazo siyo sahihi baada ya utafiti kukamilika.
Matokeo ya kutoshirikishwa kwa wakulima wadogo ni kuwapo kwa upungufu wa chakula nchini na umaskini.
Utafiti uliofanywa na taasisi iitwayo Eastern & Southern Africa Farmers’ Forum (ESAFF) kuhusu maendeleo ya kilimo na mbegu nchini ikiwalenga wakulima wadogo, ulibaini kwamba wakulima hao hawashirikishwi kwenye utafiti licha ya kuwa ni kundi muhimu kwenye sekta hiyo.
Vilevile utafiti huo ulibaini idadi ya kampuni zinazofanya biashara ya mbegu nchini, zimekuwa zikiongezeka tangu mwaka 2005, lakini wakulima wamekuwa hawafikiwi na huduma hiyo. Mwaka 2005 kulikuwa na kampuni 16, lakini sasa zimeongezeka na kufikia zaidi ya 55 wakiwamo wafanyabiashara mbegu za kilimo.
Wadau kilimo nchini, wanaamini kwamba endapo wakulima watashirikishwa kwenye utafiti, ni rahisi watafiti kubaini mahitaji yao na kutekeleza ushauri wa kiutaalamu unaotolewa na watafiti.
Mdau kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine (Sua), Dk Damian Gabagambi anasema watafiti wamekuwa hawatengi muda wa kutosha kwa ajili ya kuwashirikisha wakulima wadogo kwenye tafiti mbalimbali na matokeo yake wamekuwa hawatekelezi ushauri wa kitaalamu unaotokana na tafiti zao.
“Kwa mfano, wilayani Mbozi, wakulima walikataa mbolea waliyopelekewa na Serikali kwa kuwa hawakuelimishwa umuhimu wake ingawa utafiti ulibaini kwamba mbolea hiyo ilikuwa nzuri kwa wakulima wa wilaya hiyo,” anasema Dk Gabagambi.
Dk Gabagambi anabainisha kuwa serikali ilipata hasara kwa kuwa mbolea hiyo haikutumika na pia fedha zilizotumika kwa ajili ya kuandika ripoti ya matokeo ya matumizi ya mbolea hiyo, zilipotea.
Anasema kutokana na wakulima wadogo kutoshirikishwa kwenye tafiti za kilimo, imekuwa vigumu kutekeleza mpango wa Kilimo Kwanza.
“Tulifanya utafiti hivi karibuni kuhusu mbolea. Moja ya mambo tuliyobaini katika bajeti ya 2012/13, ni kwamba asilimia 40 mpaka 70 ya mbolea ya ruzuku ilisambazwa kwa wakulima vijijini,” anasema Dk Gabagambi.
“Kama wakulima wakishirikishwa ipasavyo katika mpango wa Kilimo Kwanza wangehoji kwanini pembejeo hazikuwafikia vijijini, anasema Dk Gabagambi. Lakini hawahoji kwa kuwa wanaamini Kilimo Kwanza ni mpango wakulima wakubwa hasa wafanyabiashara.
Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Mtandao wa Wakulima Wadogo mkoani Morogoro, Marcelina Kibena anasema wakulima wadogo wamekuwa hawashirikishwi katika tafiti.
“Kwa mfamo, hivi sasa wakulima wanaamini kuwa Kilimo Kwanza kilianzishwa na wafanyabiashara kwa ajili ya kupata soko la uhakika huku serikali ikiamini wakulima wadogo ni watekelezaji wa matokeo ya utafiti na kusahau kwamba haikuwashirikisha katika hatua za awali,” anaeleza Kibena.
Makamu mwenyekiti huyo anasema pia wakati wa kutunga sera za kilimo, wakulima wadogo wamekuwa hawashirikishwi na badala yake wamekuwa wakiambiwa watekeleze sera hizo.
Vilevile anasema serikali imekuwa ikifanya makosa kwa kuongeza bei ya pembejeo huku maisha ya wakulima yakindelea kuwa magumu.
“Mbali ya taarifa za serikali, maisha ya wakulima hayajabadilika, maisha yetu yako palepale, naamini mambo yatabadilika kama wakulima watashirikishwa kwenye tafiti.
“Ukitaka kujua mpango wa Kilimo Kwanza umewalenga wafanyabiashara na siyo wakulima, angalia jinsi kampuni mbalimbali zinavyouza pembejeo za kilimo.
“Hawa wafanyabiashara wameweka mikakati ya kuwalazimisha wakulima kununua mbegu zao, kila mwaka huku serikali ikisahau kwamba kuna mbegu za asili ambazo zinaweza kutumika,” anaeleza Kibena.
Kwa mtazamo mwingine, Kibena anasema wakulima wamekuwa hawajui umuhimu wa tafiti zonazofanyika kutokana na watafiti kutembelea maeneo vijijini bila kuchukua maoni ya wakulima.
Taasisi ya Mbegu nchini (TASTA) ambayo inawakilisha kampuni mbalimbali zinazofanya biashara ya mbegu, imekuwa ikishindwa kudhibiti vikwazo vinavyokabili sekta ndogo za kilimo nchini, hivyo tatizo hilo linapaswa kutatuliwa.

Post a Comment

 
Top