Watanzania tumekuwa wepesi mno kulalamika na kutaka maendeleo
wakati huohuo tunashiriki kwa kiasi kikubwa katika kukwamisha juhudi
hizo za maendeleo.
Kila siku kumekuwepo kelele za matatizo na kero
mbalimbali ambazo tumekuwa tukiinyooshea kidole serikali bila kujua kuwa
sehemu kubwa ya matatizo hayo inasababishwa na sisi wenyewe.
Mfano mzuri katika hili ni tatizo la foleni katika
barabara nyingi hususani jijini Dar es salam chanzo kimoja wapo kikiwa
ni biashara ndogondogo na shughuli zinazoendelea kandokando ya barabara
hizo.
Awali ilikuwa ikionekana katika baadhi ya maeneo
hususani, Kariakoo lakini siku hizi biashara za kandokando ya barabara
zinaonekana kukithiri katika maeneo mengi ya jiji.
Ukipita maeneo ya Buguruni, Ilala, Mbagala,
Mwenge, Kigogo, Manzese, Ubungo na sehemu nyingine ni jambo la kawaida
kabisa kukuta wafanyabiashara wakiwa wameingia kabisa katika hifadhi ya
barabara na kuendesha shughuli zao.
Katika kituo cha daladala cha Mwenge na Ubungo
tatizo hili linaonekana kuwa kubwa zaidi kwani uwingi wa biashara katika
maeneo hayo huchangia msongamano mkubwa wa magari na watu, hali
inayosabisha pia ongezeko la wizi na vitendo vya kihalifu.
Nyakati za usiku, hali huwa mbaya zaidi kwa kuwa
wafanyabishara wengi hujitokeza nyakati hizo kuwinda wateja kwa lengo la
kukwepa ushuru mchana hivyo kusababisha msongamano mkubwa.
Mbaya zaidi kuna wakati bidhaa hizo huangukia
barabarani hivyo muuzaji kulazimika kuziokota wakati huohuo magari
yakiendelea kupita, hali inayochangia kwa kiasi kikubwa kusababisha
foleni.
Pamoja na kusababisha foleni, hali hii inaweza pia
kuhatarisha maisha ya wafanyabiashara na hata wateja wanaofika katika
maeneo hayo kununua bidhaa.
Suala hili linaweza kuonekana la kawaida, lakini
kwa kiasi kikubwa linaweza kusababisha madhara makubwa kiuchumi na hata
kupoteza nguvu kazi ya taifa kutokana na ajali ambazo zinaweza
kusababishwa na biashara hizo.
Licha ya mara kadhaa serikali kupiga marufuku
ufanyaji wa biashara katika maeneo hayo bado zimekuwa zikiendelea na
kushamiri kwa kasi kana kwamba zinaruhusiwa kisheria.
Hata inapojaribu kuchukua hatua zaidi na kuwaondoa
katika maeneo hayo wamekuwa wakipotea kwa siku chache lakini baadaye
hurudi na kuendelea na shughuli zao kama kawaida.
Inawezekana kabisa wahusika wakawa wanafanya hivi wakidhani
wanaikomoa serikali lakini ukweli ni kwamba hata wao wanahatarisha
maisha yao na biashara zao kwa ujumla.
Endapo gari litapita kwa mwendo kasi na kuharibu
biashara au mfanyabiashara sidhani kama serikali itakuwa inahusika kwa
namna yoyote ile hivyo mhusika atakuwa ameingia katika hasara ambayo
ingeweza kuzuilika.
Tumekuwa tukisifu nchi za watu wapo makini katika
miji yao ndiyo maana inaonekana vizuri tunapoona kwenye runinga au wale
waliopata bahati za kwenda huko lakini hatuwezi kufanikiwa kufikia hali
hiyo kama hata tunashindwa kukomesha biashara katika maeneo
yasiyostahili.
Nasema hivyo kwa kuwa tumekuwa tukitamani kwa
kiasi kikubwa kupata maendeleo bila kushiriki kwa namna yoyote ile
katika kufanikisha hilo.
Lakini tukishirikiana kwa pamoja tunaweza
kulimaliza kabisa tatizo hili na kulifanya Jiji la Dar es salaam kuwepo
katika mazingira yanayostahili ukilinganisha na miji mingine mikubwa
Afrika na duniani kwa jumla.
Post a Comment