0



UNAMKUMBUKA yule beki wa Prisons aliyemkaba Amissi Tambwe mwanzo mwisho hadi wakapasuka vichwa wote wawili?
Simba imefanya naye mazungumzo na inataka kumsajili awasaidie Joseph Owino na Donald Mosoti.
Huyo si mwingine bali ni beki wa kati wa Prisons, Nurdin Chona ambaye alimkaba ipasavyo Tambwe katika mechi ya Ligi Kuu Bara ya raundi ya pili iliyochezwa Uwanja wa Sokoine, Mbeya na timu hizo kutoka suluhu.
Simba haina beki wa uhakika wa kati inayeweza kumtumia endapo mmoja kati ya Owino au Mosoti akiumia, hivyo haraka ikafanya mazungumzo ya siri na Chona ili iweze kumsajili.
Akizungumza na Mwanaspoti, Chona alisema: “Viongozi wa Simba walinifuata na kufanya mazungumzo nami, sikutaka kuwadanganya niliwaambia ukweli kwamba bado nina mkataba na Prisons na kama wananihitaji wawasiliane na uongozi ili kujua tunafanyaje.”
Chona ambaye ni askari magereza, alisema anapenda kujiunga na Simba ili apate changamoto mpya lakini hawezi kukubaliana na njia zilizotaka kutumiwa na wana Msimbazi kwani anaheshimu mkataba wake.
“Wasiogope wafuate taratibu kwa kuzungumza na uongozi na mambo yataenda vizuri,” alisema Chona.
Kwa sasa, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe hayupo nchini, lakini Katibu Mkuu wa timu hiyo, Ezekiel Kamwaga alisema: “Kila kitu cha usajili wa Simba kitawekwa wazi wiki ijayo.”

Post a Comment

 
Top