0

Kocha Hans Pluijm  

SI utani, Kocha Hans Pluijm ameihakikishia kuiletea timu yake ya zamani ya Yanga kocha mpya atakayefuata na kuiendeleza misingi aliyoiacha ili timu hiyo iendelee kutisha ndani na nje ya nchi kwa soka la uhakika.
Kabla hajapeana mkono wa kwaheri na Yanga, Pluijm aliyeifundisha timu hiyo kwa siku 107, aliwaambia viongozi wa timu hiyo kwamba atahakikisha anawaletea bonge la kocha atakayeifanya timu hiyo iwe tishio.
Pluijm raia wa Uholanzi aliyejiunga na Al- Shoalah ya Saudi Arabia, kabla ya kuondoka nchini juzi Alhamisi, aliliambia Mwanaspoti kuwa: “Nimewaambia Yanga watulie, nawaletea bonge la kocha atakayewapa mafanikio kama waliyotaka kutoka kwangu.”
“Kuna kocha naendelea kuzungumza naye na tupo katika hatua nzuri, mambo yakikaa vizuri ndiye nitakayempeleka Yanga akaendelee nilipoishia mimi, naipenda Yanga na sitaki kuona inaangukia katika mikono ya kocha mwenye kiwango cha chini yangu au asiyeweza kazi.”
Yanga imeshika nafasi ya pili katika msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara chini ya Pluijm hivyo mwakani itacheza Kombe la Shirikisho Afrika, pia ligi kuu.
Pluijm anasisitiza vitu ambavyo atahakikisha kocha mpya anakuwa navyo: “Kwanza nataka ambaye atasimamia nidhamu kwa karibu ili timu iweze kuongozwa, si mchezaji anafanya mambo atakavyo na muda anaotaka. Lazima wawe kitu kimoja hivyo kocha mpya lazima aendelee kuifuatilia nidhamu maana wachezaji wa Kiafrika bila kuwa makini na nidhamu huwezi kufanikiwa.
“Pili, ni kuifanya timu iendelee kucheza soka la kuvutia na kufunga mabao ambayo yataonekana na kila mtu kuanzia linavyoanza kutafutwa hadi linafungwa.
“Tatu, kocha mpya anatakiwa kuwa na hamu ya kuhakikisha wanafikia malengo ya kufika mbali katika ligi pamoja na michuano ya Caf (Kombe la Shirikisho), maana hiyo ni nafasi adimu kwa kocha,” alisema Pluijm anayetarajiwa kuwasili nchini kuanzia kesho Jumapili.
Kiboko ya Kavumbagu
Baada ya kumaliza kusaini mkataba Saudi Arabia, Pluijm ataelekea Ghana ilipo familia yake na atafanya mazungumzo na straika mpya aliyepanga kumleta Yanga kuchukua nafasi ya Didier Kavumbagu aliyejiunga na Azam FC.
“Nataka kuiacha Yanga ikiwa na straika anayefunga kwa njia yoyote akiwa katika mazingira yoyote, yupo mmoja wa Ghana ambaye nilianza mazungumzo naye na nikifika huko namalizana naye,” alisema.
Pluijm pia atazungumza na kiungo mshambuliaji mmoja wa Ghana ambaye amependekeza asajiliwe Yanga ili kuimarisha kikosi cha timu hiyo na kukifanya kitishe.
Wagana kumfukuza HamisKiiza
Kama Yanga ikifanikiwa kuwasajili wachezaji hao wawili sambamba na Mbuyu Twite, itakuwa imetimiza idadi ya wachezaji sita wa kigeni, wengine ni Haruna Niyonzima, Hamis Kiiza na Emmanuel Okwi.
Kanuni za TFF zinaruhusu wachezaji watano tu wa kigeni katika timu, hivyo Yanga italazimika kupunguza mmoja.
Pluijm alimtaja Kiiza kuwa ndiye atakayepunguzwa kwani anamfanya Okwi kutowajibika uwanjani.
Uongozi wa Yanga
Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga, Abdallah Bin Kleb alisema: “Tusingeweza kumzuia Pluijm kuondoka, kwa sasa ni vigumu kuzungumzia kwa undani kuhusu kocha mpya kwani tunaweza kuwanyima fursa makocha wengine kutuma maombi ya kutaka kuifundisha timu yetu. Lengo letu ni kuwa na mtu atakayeendelea pale alipoachia Pluijm na tufanikiwe.

Post a Comment

 
Top