Hussein Jumbe akiwa kazini
Ni huzuni. Kumbi za muziki wa dansi ziko tupu. Bendi maarufu
karibu zote zilizotamba miaka ya 70 na 90 zimebaki kuwa historia. Chache
zilizokuwapo tunashuhudia wanamuziki wake wakipigia viti vitupu katika
baa za kawaida kabisa, zilizopo pembezoni mwa jiji la Dar es salaam.
Nini kimetokea kwa muziki huu ambao unabakia kuwa
alama pekee na miongoni mwa burudani ambazo Watanzania wana kila sababu
ya kujivunia, kutokana na historia kuonyesha kuwa muziki huo uliasisiwa
nchini Tanzania na ulianzishwa katika Jiji la Dar es Salaam zaidi ya
miaka 80 iliyopita.
Kati ya wanamuziki wakongwe nchini, Hussein Jumbe
aliyewahi kupigia bendi za Msondo Ngoma na DDC Mlimani Park anapingana
na wanamuziki wenzake wanaoamini kuwa muziki huo unaangushwa na vyombo
vya habari.
Mfano wa kuigwa kuonyesha kuwa muziki huo bado
unakubalika, ni kile alichokifanya Jumbe, akiwa na bendi yake ya Talent
wiki iliyopita katika Ukumbi wa Kisumba zamani Sugar Ray uliopo maeneo
ya Temeke.
Jumbe alifanya uzinduzi wa albamu ya ‘Kiapo Mara
Tatu’, lakini akafanya maandalizi kama ambavyo wanafanya wanamuziki wa
sasa kama vile Jahazi Modern Taarabu, Twanga Pepete, Linah Sanga,
Diamond Plutnamz kwa kualika watu wengine wenye mvuto wanapokuwa
wanazindua albamu zao.
Kama ilivyo kawaida yake, Jumbe licha ya kuwa ni
mwanamuziki wa zamani aliachana na uzamani na kuonyesha kuwa kulialia
kwamba wanamuziki wa zamani hawasaidiwi siyo dawa.
Lakini kitu kilichofanya shoo hiyo ivutie zaidi na
kujiweka katika soko la muziki kama wafanyavyo wanamuziki wengine,
aliweka burudani tofauti tofauti ikiwamo kikundi cha muziki wa asili cha
Hayahaya Ngoma Afrika kutoka Kijiji cha Makumbusho, jijini Dar es
Salaam. Kama hiyo haitoshi katika kuwavutia mashabiki wa muziki wa aina
zote, hakuwatenga wadau wa taarabu kwani mwanamuziki wa miondoko hiyo
Isha Mashauzi alikuwapo kuwakilisha.
Cha kufurahisha ni kwamba Isha Mashauzi, akiwa na
kundi zima la Mashauzi Classic hakumuangusha kwani walifanya kile
mashabiki walichokuwa wanakikusudia, ikiwamo kuimba muziki wa taarabu
kwa ustadi mkubwa na kuimba nyimbo za wanamuziki wa muziki wa kizazi
kipya ikiwamo wimbo ‘Maneno maneno’, wa mwanamuziki Ben Pol na kuuimba
kwa ustadi mkubwa. Pia wimbo wa Injili wa mwanamuziki Bahati Bukuku‘
uitwao ‘Waraka wa Amani’ na nyimbo mbili za mwanamuziki Jumbe ambazo ni
‘nachechemea na ‘siri ya nini’.
Jumbe anena
Mwanamuziki huyo mkongwe alisema kuwa
alichokifanya ni kusoma mahitaji ya soko la muziki wa sasa na kujua
mahitaji ya wadau wa burudani na hatimaye hadi leo anapiga muziki na ana
mashabiki vijana kwa wazee. “Niliwahi kusema kulalamika siyo dawa,
tulijisahau miaka ya 80-90, tulijisahau na vijana wamechukua nafasi
wanaifanyia kazi. Tunachotakiwa kufanya sasa ni kuhakikisha tunaurudisha
muziki wa dansi kwenye chati ingawa kazi kubwa inatakiwa kufanyika,
”anasema Jumbe.
Jumbe anafafanua kuwa licha ya vyombo vya habari
kuusahau muziki huo na wanamuziki wenyewe wanataka ujiuze kwa umaarufu
wa zamani bila kujali dunia inazunguka na inakwenda sambamba na
mabadiliko.“Hata Serikali imefanya mabadiliko, kulikuwa na Chama kimoja
na sasa ni vyama vingi na muziki vivyo hivyo unatakiwa uende na kasi ya
mabadiliko, ”anasisitiza Jumbe.
Jumbe ambaye wimbo wake wa ‘Kiapo Mara Tatu, ambao
ndiyo umebeba jina la albamu hiyo, uliingia kwenye kinyang’anyiro cha
tuzo za Kilimanjaro Music, katika kipengele cha Wimbo bora wa Kiswahili,
ingawa haukufanikiwa kupata tuzo hiyo.
Wadau wanasemaje?
Mohamed Kambangwa, anasema miongoni mwa vitu
vinavyomsikitisha ni wanamuziki wa muziki huo, kutaka watukuzwe kwa yale
waliyoyafanya zamani bila kufanya kipya ilihali uwezo wa kufanya hivyo
wanao.
“Wanataka redio ambazo nyingi ni za biashara
zipige nyimbo zao za zamani na kuacha kupiga mpya, badala ya kufanya
kitu kipya ili kifufue ya zamani, “anasema Kambangwa. Mwanaidi Juma,
anasema kuwa anaamini muziki wa dansi wa zamani ni bora kuliko wa sasa,
lakini akiwataka wanamuziki wa muziki huo kuacha kubweteka na kulia
wasaidiwe na Serikali bila kujibidisha kuhakikisha muziki wa dansi hasa
usiokuwa na masebene ya Kikongo unapanda chati.
Raymond Ayoub, anasema wadau wa muziki
wanachanganya muziki wa zamani na dansi, huku akifafanua kuwa muziki wa
zamani ni wa bendi kama za Cuban Marimba, Moro Jazz, Kiko Kids, lakini
muziki wa dansi unatakiwa uendelee kuwapo.
“Wanamuziki wa zamani wanataka kuendelea kufanya
vizuri wakitumia nyimbo zile zile za zamani kama Jojina, Rangi ya
Chungwa, Mama Bembeleza Mwana, Kitambaa Cheupe, nyimbo ambazo kwa sasa
wanaozifahamu na kutambua thamani yake ni wachache, wanatakiwa kutunga
nyimbo mpya,” anaongeza Ayoub.
Wanamuziki wa enzi za Jumbe na wanaopiga muziki wa dansi
Mwanamuziki mkongwe wa bendi ya Msondo, Saidi
Mabera, anasema kuwa licha ya kufanya juhudi binafsi kama ambazo wao
kama Msondo wamekuwa wakifanya, bado kuna haja ya vyombo vya habari
kuwaunga mkono. Anafafanua kuwa Jumbe anafanya vizuri, lakini kwa siku
ni mara ngapi nyimbo zake zinapigwa redioni, kibaya zaidi redio nyingi
katika vipindi vyao wanataja nyimbo ambazo wanataka ziombwe.
“Katika kipindi mtangazaji anasema nyimbo ambazo
ni ruhusa kuziomba kwa siku hiyo na ukiomba nyingine kati ya hizo
haitakuwapo. Sasa kwa watangazaji wa sasa unafikiri kuna ambaye atataja
nyimbo ya Msondo, Sikinde, kama siyo za kizazi kipya anazozifahamu,
”anasema na kuhoji Mabera ambaye amefanya kazi na bendi hiyo kwa miaka
zaidi ya 40. Hassan Rehani Bichuka kiongozi wa bendi ya Sikinde, anaanza
kwa kumlaani aliyeanzisha mpango maalumu wa kuua muziki wa dansi
nchini.
Anasema aliyeanzisha mpango huo alihakikisha
vyombo vya habari vinausahau na kufanikiwa hatua yake ya kwanza ambayo
ilikuwa muhimu sana kwenye mpango huo.
“Nipo kwenye tasnia hii siku nyingi, niamini
nakwambia hata tufanye nini, kuna mtu au watu hawataki muziki wa dansi
uendelee na wana nguvu za kuua na kama hakutakuwa na juhudi za
kuhakikisha haufi utakufa. Sisi bado tunapambana na ndiyo maana unaona
hizi bendi bado zipo licha ya kuwa nyimbo zetu hazipigwi redioni,
”anafafanua Bichuka.
Mwanamuziki kinda kutoka katika bendi ya Msondo,
Hassani Moshi Junior anasema; atahakikisha muziki wa dansi haufi na
ndiyo maana hakufikiria kujiunga na muziki wa kizazi kipya ambao una
fedha kwa sasa, kutokana na kuutakia mema muziki huo.
Anafafanua anaziunga mkono juhudi zinazofanywa na
baba zake kwa kufanya vitu vipya kila siku ili kuhakikisha wale
mashabiki wao wa asili wanapata burudani.
“Mimi sikubaliani na wazo la kwamba redio hazipigi muziki huu
hivyo unakufa. Kila siku kumbi zinajaa mashabiki na kila muziki
ninaamini una mashabiki wake, hata hao wanaocheza Bongofleva mwisho wa
siku wanakuja kusikiliza muziki na kupata burudani ya kweli kwenye
muziki wa dansi, “anasema Moshi Junior ambaye ni mtoto wa marehemu Tx
Moshi William aliyekuwa ni mwanamuziki wa bendi hiyo hadi anafikwa na
umauti.
Salim Zahoro kiongozi wa bendi ya Shikamoo
anazitupia lawama redio kwa kusema kuwa zimeupotezea muziki wa dansi
ndiyo maana umekuwa kimya.
“Muziki huu uliwahi kutamba lakini kuna mtu anauua
na siyo mwingine bali ni redio”anasema kwa kifupi Zahoro, aliyeanza
kuimba muziki huo zaidi ya miaka 50 iliyopita akiwa na bendi ya Kiko
Kids.
Post a Comment