0
Dar es Salaam. Idadi ya wagonjwa wanaohitaji huduma ya upasuaji katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili huenda ikapungua baada ya hospitali hiyo kupewa vifaa tiba kutoka Serikali ya Misri vitakavyotumika kutoa matibabu kwa wingi na haraka.
Zaidi ya asilimia 60 ya wagonjwa wanaohitaji huduma ya upasuaji katika Hospitali ya Muhimbili ni wenye matatizo ya urolojia hali inayoonyesha kuwa mashine hizo zitahudumia wagonjwa wengi zaidi.
Akizungumza wakati akipokea vifaa hivyo kutoka kwa Balozi wa Misri nchini, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Dk. Marina Njelekela alisema huduma ambazo hutolewa na kitengo cha urolojia ni pamoja na uvimbe wa tezi dume, kuziba kwa njia ya mkojo, saratani ya kibofu na saratani ya tezi la kiume.
Dk. Njelekela alisema vifaa hivyo vimekuja wakati muafaka ambapo vitasaidia kufikia azma ya Serikali ya kutoa huduma bora ya afya kwa wakati, kwa wingi na kwa viwango vinavyokubalika.
Akitoa vifaa hivyo, Balozi wa Misri nchini, Hossam Moharam alisisitiza kuwa nchi yake itaendelea kuisaidia hospitali hiyo kwa kuipatia vifaa tiba zaidi ili kuboresha huduma ya afya.

Post a Comment

 
Top