0

>Wachezaji wa Manchester City wakishangilia ubingwa wa Ligi Kuu England jana Jumapili. PICHA NA AFP  
MANCHESTER City imenyakua ubingwa wa Ligi Kuu England katika staili ya aina yake baada ya kuichapa West Ham United uwanjani Etihad na kuwaacha Liverpool kwenye mataa wakishangaa licha ya ushindi wao dhidi ya Newcastle United kwenye Uwanja wa Anfield jana Jumapili.
Mabao ya Samir Nasri na Vincent Kompany yalitosha kuipa ushindi wa 2-0 Man City na hivyo kunyakua ubingwa huo kwa mara ya pili katika kipindi cha miaka mitatu, huku Liverpool waliokuwa na matumaini ya kumaliza ukame wa taji hilo msimu huu wakiishia kushika nafasi ya pili baada ya kutokea nyuma na kushinda 2-1 dhidi ya Newcastle United.
Daniel Agger na Daniel Sturridge walifunga mabao ya haraka ndani ya dakika mbili na kuifanya Liverpool kujikomboa kwenye bao la kujifunga Martin Skrtel ambalo ni la nne kwa msimu huu. Man City imenyakua ubingwa baada ya kufikisha pointi 86, pointi mbili zaidi ya Liverpool.
Chelsea imeshika nafasi ya tatu kwa kufikisha pointi 82 baada ya kuishinda Cardiff City 2-1, wakati Arsenal imekamilisha timu nne za juu zitakazocheza Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao kwa kushika nafasi ya nne baada ya kuichapa Norwich City mabao 2-0. Tottenham Hotspur na Everton zimefanikiwa kupata nafasi ya kucheza Ligi ya Europa msimu ujao baada ya kushinda mechi zao, wakati Spurs waliikung’uta Aston Villa 3-0 na Everton ilishinda 2-0 ugenini kwa Hull City.
Matokeo ya mechi nyingi za mwisho za ligi hiyo zilizochezwa jana, Manchester United ilichomoa na kutoka sare ya 1-1 na Southampton, Fulham wakitoka sare ya 2-2 na Crystal Palace na Stoke City ikiishinda ugenini kwa West Bromwich Albion mabao 2-1 na Sunderland ikichapwa nyumbani na Swansea City mabao 3 -1.

Post a Comment

 
Top