0

Mgombea wa nafasi ya Urais,katika Uchaguzi Mkuu wa Klabu ya Simba,Evans Aveva (juu ya gari) akisindikizwa na mashabiki na wanachama wa klabu hiyo akielekea makao Makuu ya klabu hiyo,Mtaa wa Msimbazi,Kariakoo,Dar es salaam kwenda kuchukua fomu ya kuwania nafasi iyo.Picha na Michael Matemanga   


GUMZO la Dar es Salaam jana Jumapili ilikuwa ni Evans Aveva na Sued Nkwabi waliochukua fomu za kuwania uongozi wa Simba kwa kishindo. Vigogo hao wenye ushawishi mkubwa ndani ya Simba walisindikizwa na kundi kubwa la mashabiki na wanachama wa Simba na kusababisha mitaa ya Msimbazi kufurika kwa mbwembwe za kila aina.
Aveva anagombea nafasi ya Urais wa Simba na Nkwabi Makamu wa Rais. Hata hivyo Aveva ndiye aliyekuwa na umati mkubwa zaidi na wengi walipania kutaka kusikia atazungumza nini huku ikielezwa kwamba mpinzani wake wa karibu zaidi Michael Wambura atachukua fomu mchana huu.
Wapambe hao walikuwa wakiimba wimbo; “Tumechoka kukaa eda kwa miaka minne sasa Simba tunataka tutoke kiushindani zaidi.” Wakimaanisha kwamba wamechoka kuteseka kuwa vibonde kwa muda huo sasa wanataka Simba ya ushindani.
Maandamano  yalianzia mtaa wa Lumumba ambapo Aveva alifika hapo akiwa ndani ya gari aina ya Mercedes Benz yenye namba za usajili T840 BHQ akifika kuungana na mashabiki wanaomuunga mkono kabla ya kushuka na kupakia katika gari maalum aina ya Mitsubishi Chariot iliyompa fursa ya kuonekana kwa juu ambako aliweza kuwapungia mkono watu wote wakati akipita barabarani akielekea yalipo makao makuu ya Simba.
Msafara huo ulipitia barabara ya Uhuru na kukamata ile ya Msimbazi ambako  mbele kulikuwa na pikipiki zisizopungua 30  ambapo alipofika makao makuu ya Simba  alikutana na mamia ya mashabiki wa timu hiyo waliokuwa wakimsubiri ambako shangwe iliongezeka na kufanya zoezi hilo kufana.
Akiwa katika makao makuu ya Simba, Aveva aliongozana na wagombea wengine wa nafasi za ujumbe akiwemo Said Tully, Idd Kajuna, Ramson Rutiginga. “Umati huu ulionisindikiza ni kiashiria tosha kwamba nakubalika na nina deni kubwa kwa Wanasimba endapo nitapata nafasi hii,”alisema Aveva   
Kwa upande wa Nkwabi ambaye alikuwa mjumbe kwenye kamati ya utendaji alisema; “Ninawania Umakamu wa Rais ili kuitumikia timu kwa nguvu zaidi nikishirikiana na wanachama wengine na viongozi watakaokuwepo. Najua wanachama na mashabiki wengi wangependa kuiona Simba ikiwa kwenye makali yake ya awali kwa kusajili wachezaji makini na wenye uwezo, hivyo nitahakikisha hilo linasimamiwa.”
Nkwabi amepanga kurejesha fomu hiyo kwenye ofisi za klabu ya Simba hii leo Jumatatu na kusubiri taratibu nyingine za uchaguzi kuendelea hadi hapo Juni 24 yatakapotolewa rasmi majina ya wagombea watakaowania nafasi mbalimbali za klabu hiyo na kuruhusiwa kuanza kampeni. Mwanachama mwingine aliyechukua fomu ya makamu wa rais ni Wilbard Mayage.

Post a Comment

 
Top