0
Wanaitwa Mabaga Fresh na awali walitamba na kazi zao nyingi ambazo zilikuwa gumzo si tu kwa washabiki wa muziki wa Hip Hop, bali pia hata kwa watu wa kawaida wasio na mapenzi na aina hiyo ya muziki.
Wimbo kama Ngangari, Tunataabika, Mtulize, Mtu bee, Mauzauza, Fagio la chuma na zingine ambazo ziliwatambulisha vyema katika ulimwengu wa muziki na kuwaweka kileleni katika chati mbalimbali za Hip Hop.
Hali hiyo ilikuwa inajitokeza huku kukiwa na ushindani mkali wa makundi ambao ulinadhifishwa na majibizano ya wasanii kwa wasanii na kundi kwa lingine hali ambayo ilichochea utamu wa muziki huo na kuzoa halaiki ya washabiki.
Makundi yaliyokuwa yakitamba siku hizo ikiacha Mabaga Fresh ni pamoja na Gang Star With Matatizo G(WM), TMK Wanaume, BDP, Gangwe Mob, Watengwa, Walume Ndago na East Coast Team.
Mengine ni Unique Sisters, Wateule na makundi mengine ambayo yalikuwa gumzo kubwa kutokana na kazi zao achilia mbali wasanii binafsi ‘solo artist’ ambao hata hivyo walilazimika kuibukia katika moja ya makundi hayo ingawa hawakuwa wanachama wa kudumu.
Mmoja kati ya wasanii hao ni Zay B aliyeimba na Mabaga Fresh wimbo ‘Nipo Gado’ ambapo alijitambulisha kama mwanadada gaidi akiwaponda Gangwe Mob ambao walikuwa chini ya Inspekta Haroun.
Muziki wa makundi hayo ulivutia wengi na kufanya hata wale waliokuwa wakiuchukulia kuwa ni wa kihuni kutafakari mara mbili na kubadili mwelekeo.
Kundi hilo ambalo lilikuwa linaundwa na Christoms Mwingira ‘Dj Snox’ na Jumanne Omary ‘Mkuu wa Majeshi’, hivi sasa limejipanga na tayari lina nyimbo 30 na kati ya hizo ambazo zimerekodiwa kwa ajili ya kuwepo katika albamu hiyo ni 14. “Tumejipanga na mashabiki wa muziki wa Hip Hop wajipange” anasema Dj Snox na kuongeza kuwa albamu moja kuwa na nyimbo 14 ni jambo geni bongo lakini la kawaida nchi za Marekani na Ulaya” anasema Mwingira.
Anasema albamu itaitwa 770 na wataisimamia wenyewe kimauzo ili kuona jinsi gani itawalipa tofauti na siku za nyuma ambapo waliwatumia mawakala ambao walikuwa wanachangia kupotea kwa mapato yao.
Snox anasema ukimya wao haukuwa wa bure na walikuwa wanafanya kazi ingawa hawakupata muda wa kurekodi au kuzifanya ziwe hewani na baada ya kujiweka sawa sasa wanakuja.
“Tulikuwa chimbo (kambini) kiaina ingawa kila mmoja kwa wakati wake alikuwa anapata fursa ya kushiriki na makundi tofauti na muziki,” anasema na kuongeza kuwa madai kuwa kinachokuja sasa ni tofauti.
Msanii huyo alikataa kuzielezea kwa undani nyimbo zao na kudai kuwa hakuna ambayo itamlenga mtu na kama ikitokea basi itakuwa ni mtazamo wake lakini sicho walicholenga wao.
Anasema kundi hilo ambalo lina sifa kubwa ya kuwakabili wapinzani wao majukwaani kwa kutumia mashairi ya nyimbo zao hivi sasa linakuja tofauti.
“Wakati wa bifu umekwisha kaka hivi sasa ni kazi na kuiamsha jamii kwani inasongwa na mambo mengi” anasema Mwingira na kuongeza kuwa ufadhili ma sasapoti ya wadau inahitajika kwani pamoja na yote pekee yao hawawezi.

Post a Comment

 
Top