0
Dar es Salaam. Kamati ya maadili ya uchaguzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) bado haijatoa ripoti rasmi ya wagombea ambao walienguliwa kwenye kinyang’anyiro cha uchaguzi huku kukiwa na taarifa kuwa baadhi ya wagombea hawatarudishwa kwenye kinyang’anyiro hicho.
Habari ambazo Mwananchi ilizipata zinasema kuwa licha ya kamati ya maadili kuwasafisha, bado haijawasilisha rasmi ripoti yake kwa maandishi, lakini TFF imekuwa ikigomea kurejeshwa kwa wagombea hao.
“Kilichotokea ni kwamba kamati imewasafisha, lakini haijawarejesha kwenye kinyang’anyiro, kusafishwa ni suala lingine na kurudishwa ni suala lingine,” kilisema chanzo kimoja kutoka ndani ya TFF na kuongeza:
“Suala kama la Rukambura, katiba ya TFF inaeleza wazi mtu akienda mahakamani anaondolewa kujihusisha na masuala ya soka, sasa kamati inamsafishishaje? haiwezekani wakarudishwa wote, kinachosubiriwa ni huo uamuzi wa maandishi kutoka kamati ya maadili na hatua nyingine zitafuatwa.”
Hivi karibuni wagombea saba  walioenguliwa kwenye kinyang’anyiro cha uchaguzi na kamati ya  uchaguzi ya TFF iliyo chini ya Hamidu Mbwezeleni kwa kile kilichoelezwa kuwa hawana hatia walirudishwa.
Wagombea hao ni Kilungeja Nazarius, Riziki Juma, Wilfred Kidau, Shaffih Dauda, Omary Abdukadir na Richard Rukambura.

Post a Comment

 
Top