Timu ya Taifa Stars ikiwa nchini Gambia
Banjul, Gambia. Safari ya Timu ya Taifa (Taifa Stars), juzi
usiku ilikumbana na misukosuko ya aina yake baada ya kukwama majini
ndani ya kivuko kwa zaidi ya saa tano wakati ikielekea Mji Mkuu wa
Gambia, Banjul.
Stars inayodhaminiwa na TBL, ilikwama majini baada
ya kivuko walichokuwa wakitumia kutoka kwenye mpaka wa nchi hiyo na
Senegal, kushindwa kuendelea na safari kutokana na kuzidiwa na mkondo wa
maji.
Kutokana na hali hiyo, kivuko hicho kinachofanana
na kile cha Mv Kigamboni, kililazimika kukwepa mkondo huo wa maji kwa
kupitia njia nyingine, lakini nako kilishindwa kuendelea na safari na
kusimama majini mpaka mpaka kilipokuja kuvutwa na chombo kingine mpaka
kwenye bandari.
Mbali na hali hiyo, Stars, leo inahitimisha dakika
tisini za safari iliyokosa tija kucheza fainali za Kombe la Dunia
mwakani, kwa kupambana na Gambia katika mchezo wenye taswira ya
kukamilisha ratiba.
Siyo Tanzania wala Gambia itakayofaidika na
ushindi kwenye mchezo huo, kwani zote zimeshaondoka kwenye vita ya
kuwania tiketi ya kucheza fainali hizo mwakani nchini Brazil.
Kikubwa kwa timu hizo leo ni kulinda heshima,
lakini zaidi Gambia wakitaka kulipa kisasi cha kufungwa mabao 2-1 na
Tanzania katika mchezo wa kwanza uliochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar
es Salaam.
Kabla ya mchezo wa leo, Stars ilishinda mechi
mbili tu, dhidi ya Morocco (3-1), na kisha dhidi ya Gambia (2-1). Mechi
zote imeshinda kwenye uwanja wa nyumbani.
Taifa Stars ilipoteza mechi zake dhidi ya Ivory
Coast nyumbani na ugenini (2-0 ugenini) na (4-2 nyumbani), kisha
ikakubali kipigo cha mabao 2-1 ugenini nchini Morocco.
Kwenye msimamo, Stars iko nafasi ya tatu ikiwa na
pointi sita, wakati wapinzani wao, Gambia wanaburuta mkia Kundi C wakiwa
na pointi moja. Ivory Coast tayari imefuzu hatua ya mtoano.
Mshindi kutoka kila kundi kati ya matano hatua ya
mtoano, atafuzu kucheza fainali hizo, ambazo kwa mara ya kwanza
zitachezwa nchini Brazil.
Stars ilitua mjini Banjul katikati ya wiki hii,
huku Kocha Kim Poulsen akisema wazi kuwa anaupa uzito wa kutosha mchezo
dhidi ya Gambia hata kama wakishinda hawatakwenda popote.
Kocha wa Stars, Kim Poulsen alisema pamoja na
kushindwa kufuzu kwa fainali hizo mchezo huo ni muhimu kushinda kwa vile
kumaliza nafasi ya pili kwenye kundi kutaisaidia kupanda viwango.
Mechi hiyo itakayopigwa kwenye Uwanja wa Independence mjini
Bakau, unatarajiwa kuchezeshwa na mwamuzi wa kati kutoka nchini Rwanda,
Hudu Munyemana.
“Tukishinda na kupanda viwango vya ubora, kutatupa
fursa ya kupangwa kwenye kundi zuri kwenye hatua ya kufuzu kwa fainali
zijazo za Afrika,” alisema Kocha Poulsen.
Stars itawategemea Mrisho Ngassa, Juma Kaseja,
David Luhende, Henry Joseph, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Frank Domayo na
Erasto Nyoni kutengeneza matokeo mazuri ugenini.
Kwenye kikosi hicho, hawatakuwemo washambuliaji
Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu baada ya kuzuiwa na klabu yao ya TP
Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Kwa upande wa Gambia, imewaita wanasoka wake saba
wanaocheza soka la kulipwa nje ya nchi, ambapo kufikia juzi nusu
walishawasili na kujiunga na wenzao tayari kwa mchezo huo.
Kocha wa Gambia, Peter Bonu Johnson alisema
amefurahishwa kuwasili kwa wachezaji, Omar Colley, Ken Mansally na Demba
Savage kutoka Ubelgiji, na kwamba alikuwa akiwategemea Momodou Ceesay
na Tijan Jaiteh jana.
Post a Comment