Kaze na Tambwe waliumia Jumamosi iliyopita wakati Simba ilipoikabiri Mbeya City na kutoka sare ya 2-2.
Dar es Salaam. Benchi la ufundi
la Simba limeshusha pumzi kufuatia wachezaji wake wawili wa kimataifa
raia wa Burundi, Gilbert Kaze na Hamis Tambwe kurejea uwanjani baada ya
kupona majeraha waliyopata Jumamosi iliyopita wakati wakiitumikia timu
hiyo ilipokuwa ikipambana na Mbeya City kwenye Uwanja wa Taifa jijini
Dar es Salaam.
Katika michezo huo uliokuwa na ushindani mkubwa,
timu hizo zilitoka sare ya 2-2, mabao yote ya Simba yalipachikwa wavuni
na Hamis Tambwe ambaye hadi sasa ameshazifumania nyavu mara sita katika
mechi tatu za Ligi Kuu alizoitumikia klabu hiyo.
Kwa mujibu wa Daktari wa Simba, Yassin Gembe
alisema kuwa wachezaji hao walipatwa na matatizo hayo katika mechi hiyo
ambapo Kaze alishtuka Nyonga na Tambwe aliumia nyama za paja.
Alisema hivi sasa wanendelea vizuri na jana
wameanza mazoezi mepesi hivyo ana imani kuwa hadi kufikia Jumamosi
watakuwa wapo fiti tayari kwa kukalinana na vijana wa JKT Ruvu katika
mchezo wa Ligi Kuu utakaofanyika kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es
Salaam. Hata hivyo mbali na wachezaji hao kurejea uwanjani, Gembe
alisema kuwa kuna uwezekano mkubwa kwa timu hiyo kumkosa kiungo Henry
Joseph ambaye anasumbuliwa na maumivu ya goti.
“Hali ya Henry bado kidogo hajakaa sawa, lakini
kuanzia kesho (leo) tunaweza kujua anaweza kuanza lini mazoezi ila Tambe
na Kaze wao wapo vizuri na leo jioni (jana) watanza mazoezi,”alisema
Gembe.
Timu ya Simba imepiga kambi yake katika hoteli ya
Bamba Beach iliyopo Kigamboni jijini Dar es Salaam ikijifua kwa ajili
ya mchezo wake wa Jumamosi wa Ligi Kuu dhidi ya JKT Ruvu, ambapo
inahitaji ushindi ili izidi kujikita juu kabisa ya msimamo wa ligi hiyo.
Post a Comment