Baadhi ya wachezaji wa kikosi kipya cha klabu ya Simba.
WACHEZAJI wa Simba raia wa Burundi, beki
Gilbert Kaze na straika Tambwe Amis walitua Dar es Salaam jana Jumatatu
saa sita usiku, lakini Tambwe amerusha kombora na amewatamkia mashabiki
wa Simba kwamba atafanya zaidi ya straika.
Tambwe anaongoza kwenye chati ya ufungaji bora
katika ligi ya Burundi akiwa na mabao 22 huku anayemfuata akiwa na mabao
13 na kila timu imebakiza mechi mbili kumaliza msimu.
Mchezaji huyo alizungumza na Mwanaspoti
jana Jumatatu jioni kwa simu akiwa kwenye Uwanja wa Ndege wa Bujumbura
na kusema; “Nimefanya mazoezi ya kutosha na Vital’O kwenye siku ambazo
nilikuwa Burundi, ndio maana nakwambia kwamba niko fiti kimazoezi.
“Tulikuwa na mechi ya ligi Jumapili dhidi ya
Academie Tchite tukashinda mabao 3-0, lakini mimi sikucheza kwa vile
nilitaka mwili upumzike kwa kuwa nina kazi nzito sana naianza na Simba
wiki hii, natakiwa mwili upumzike kidogo.
“Ila Kaze yeye alicheza hiyo mechi na yuko vizuri
vilevile. Najua Simba wamenigharimia ndio maana nataka nije nitulie
nifanye kazi zaidi ya hii niliyokuwa nafanya hapa Vital’O. Nazijua timu
za Tanzania kama Azam, Yanga, Kagera, Mtibwa na Coastal Union ndio maana
sina wasiwasi sana na ligi ya Tanzania.
“Nakuja kucheza kama straika namba 9 kazi yangu ni
kufunga mabao tu, naomba Mungu anisaidie tu nisiumie. Ila nitakuja
kuonyesha utofauti kwa vile najua Simba wameninunua wakanitoa Burundi
kuja kufanya kazi, nahitaji kuonyesha utofauti. Naomba tu Mungu
aisimamie miguu yangu na akili yangu,”alisema straika huyo.
Akizungumzia utata wa uhamisho wao alisema: “Kuna
malipo kidogo ya kumalizia mkataba ambayo Simba wanatakiwa kuwalipa
viongozi wa Vital’O lakini si kiasi kikubwa. Viongozi wametwambia kwamba
tusiwe na wasiwasi tuje Dar es Salaam ndani ya kipindi kifupi
watamalizana na tutacheza.
“Tukishafika tutakwenda moja kwa moja Tabora
kuanza mazoezi na timu kujiandaa na mechi ya Jumamosi (dhidi ya Rhino
Rangers) najua mambo yatakwenda sawa na tutajitahidi kufanya kwa nguvu
ili kutafuta namba na kuhakikisha Simba itafanya vizuri, huo ndio
mkakati,”alisisitiza kwa kujiamini huku akilalamikia hali ya hewa ya
sasa ya mvua mjini Bujumbura, Burundi.
Katibu Mkuu wa Simba, Evodius Mtawala aliliambia Mwanaspoti
jana Jumatatu kwamba; “Wakiamka tu leo Jumanne watasafiri kwenda Tabora
kujiunga na timu tayari kwa maandalizi ya msimu. Ni wachezaji wazoefu
ambao haitawachukua muda mrefu sana kuelewana na wenzao.”
Ujio wa wachezaji hao unafanya Simba iwe na
wachezaji wanne wa kigeni huku ikiacha nafasi moja ya straika wa Uganda,
Moses Oloya ambaye wamepanga kumsajili kwenye dirisha dogo. Wachezaji
wengine wa kigeni walioko Simba ni raia wawili wa Uganda, Abel Dhaira na
Joseph Owino.
Kama hesabu za benchi la ufundi zikienda sawa
kikosi cha kwanza cha Simba msimu ujao kitakuwa hivi; Dhaira, Nassor
Chollo, Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, Gilbert Kaze, Joseph Owino, Jonas
Mkude, Amri Kiemba, Abdulhalim Humoud, Betram Mwombeki, Tambwe Amis na
Ramadhani Chombo ‘Redondo’.
Post a Comment