0

Choo maalumu cha kuhamishwa  

Uchafu wa hali ya juu…usiofaa kwa kutazama, wala kuutumia kufanya kazi fulani, umegundulika kuwa na manufaa lukuki kwa matumizi ya binadamu. Uchafu huo si mwingine bali ni kinyesi cha binadamu pamoja na mkojo.
Mfumo wa usafi wa mazingira ya kiikolojia hautiliwi maanani hapa nchini, pamoja na kufafanuliwa kwa kina na wataalamu mbalimbali, lakini bado imekuwa ni vigumu kwa Watanzania kuitilia maanani na kuitumia kwa tija.
Barani Asia, taka mwili zimekuwa zikihifadhiwa na kufanyiwa utafiti kwa miaka zaidi ya 1,000, huku mfumo huo ukilindwa katika vifungu vya sheria ya kutunza taka ya mwaka 1988, Korea ya Kusini.
Kitaalamu mfumo huo unajulikana kama Ecological Sanitation System, ambao unatumia taka mwili za binadamu na kuzirejesha katika matumizi yenye thamani huku ukitunza mazingira.
‘Taka mwili’ zinafaa kwa nishati
Mtaalamu wa Mazingira kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Fredrick Mwanuzi anasema kama usimamizi wa mazingira utazingatiwa basi ipo haja ya kufanyia utafiti taka mwili kwa ajili ya matumizi mbalimbali kwa sababu zina manufaa makubwa katika nyanja mbalimbali.
Mwanuzi anasema wakati umefika sasa kinyesi cha binadamu kichukuliwe kama malighafi badala ya uchafu na kutumia mbolea hiyo kwa ajili virutubisho vya kilimo, nishati, pamoja na dawa za binadamu.
“Kilo 25 hadi 50 za kinyesi huzalishwa na mtu mmoja kwa mwaka, hii ni sawa na kilo 0.55 nitrogen, 0.18 phosphorus na 0.37 potassium, vilevile binadamu huzalisha kiasi cha lita 400 za mkojo kwa mwaka ambazo huwa na kg 4.0 nitrogen, 0.4 phosphorus na 0.9 za potassium,” anasema.
Wataalamu wa mazingira nchini Tanzania walijaribu ‘taka mwili’ kuzifantia mchakato wa kitaalamu ili kuwa malighafi, walichagua eneo la Majumba Sita jijini Dar es Salaam lengo kubwa likiwa ni kuzuia kinyesi kinachotoka chooni kuchafua maji ambayo yapo ardhini.
Mtaalamu wa mazingira Esnati Chaggu alifanya utafiti na kugundua kuwa, zaidi ya asilimia 80 ya wakazi wa Jiji la Dar es Salaam wanatumia vyoo vya shimo ambavyo vinachafua maji yaliyomo ardhini huku watu wengi wanategemea maji ya visima vyenye urefu zaidi ya meta 6.75 pamoja na mabomba ambayo huathiriwa na kinyesi kinachofukiwa ardhini. “Maji yaliyoko ardhini yanaathiriwa na aina ya vyoo ambavyo Watanzania wanavitumia, asilimia 90 hutumia vyoo vya shimo.
“Tulichagua eneo la Majumba Sita ambalo lina asilimia kubwa ya visima vyenye kina kifupi na wakazi wengi wanatumia vyoo vya shimo na wengine hawana kabisa na wanajisaidia vichakani,” anasema.
Kutokana na mazingira hayo walibuni namna ya kuhifadhi kinyesi cha binadamu kwa manufaa na pia kutunza mazingira hasa maji ambayo yalisababisha mlipuko wa magonjwa ya kuambukiza kama kipindupindu na kuharisha.

Post a Comment

 
Top