0

Wafanyakazi wa kiwanda cha maziwa wakiwajibika kazini  

Kwa muda mrefu sasa, wafanyabiashara wengi wadogo wamekuwa wakilalamika kwamba kanuni lukuki na kodi kubwa zimekuwa zikichangia kudumaa kwa biashara na kuwavunja moyo wajasirimali.
Malalamiko yao yanatokana na ukweli kuwa ili mtu asajili biashara yake anatakiwa kupitia kwa mamlaka zaidi ya 11 ambazo zinatoa vibali na leseni za biashara na mchakato huo unaweza kuchukua mwezi mzima bila usajili kukamilika.
Kutokana na mlolongo huo mrefu, wadau wanapendekeza kwamba iwepo mamlaka moja ambayo itashughulikia utoaji wa vibali ili kuokoa muda na kupunguza au kuondoa usumbufu usiokuwa wa lazima.
Hivi karibuni malalamiko mengine yalitolewa na wasindikaji wa maziwa ambao nao wanaamini mamlaka zaidi ya 11 kwa mfano, Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika sekta ya maziwa zinasababisha gharama za biashara kuwa kubwa.
“Hatusemi kwamba kusiwapo na wadhibiti la, tunachohitaji ni wadhibiti wachache ambao watawasaidia wafanyabiashara wadogo kujiimarisha pia kusajili biashara zao,” anasema Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wasindika Maziwa nchini (TAMPA), Edmund Malick.
Kanuni zinatubana
Malick anasema kuwapo kwa kanuni nyingi zinazuia wajasiriamali wapya na kukwamisha juhudi za kuimarisha sekta ya maziwa nchini.
Endapo mjasiriamali anapenda kuwekeza au kuanzisha kiwanda cha kusindika maziwa cha lita 6,000, anapaswa kuwa na mtaji wa wa Sh45 milioni kabla hakijaanza kufanya kazi.
Kwa mujibu wa Malick, fedha hizo ni nyingi na wengi wa wafanyabiashara hawajui namna ya kupata fedha hizo.
Malick anasema zaidi ya lita milioni 6 za maziwa zinazalishwa nchini na wafugaji kila siku, lakini kwa sasa wasindikaji wana uwezo kutengeneza lita 300,000 kwa siku sawa na asilimia tatu ya maziwa yote yanayozaslishwa nchini.
“Badala ya kuondokana na kanuni zisizokuwa na maana ili kuwavutia wajasiriamali zaidi wenye mitaji midogo katika sekta ya maziwa, Serikali imekuwa ikiweka vikwazo vingi zaidi vya udhibiti wajasiriamali kuingia katika sekta hiyo,” anasema Malick.
Taarifa ya hivi karibuni ya Shirikisho la Wenye Viwanda nchini (CTI), inaonyesha kwamba wasindika maziwa wana mzigo mkubwa wa kulipa tozo mbalimbali za kupata ruksa ya kufanya kazi hiyo kutoka kwa wadhibiti mbalimbali wa kisekta.

Post a Comment

 
Top