Mfanyabiashara maarufu barani Afrika
Wakati vuguvugu la gesi iliyogunduliwa mkoani Mtwara lilipokuwa likiendelea, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alikuwa akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa kiwanda cha saruji kinachomilikiwa na Rais na Ofisa Mkuu Mtendaji wa Dangote Group, Alhaji Aliko Dangote.
Dangote ambaye ni bilionea amewekeza karibu Dola
500 milioni za Marekani sawa na Sh8 tilioni katika kiwanda hicho
kitakachojengwa mkoani Mtwara.
Kiwanda cha Dangote kinatarajiwa kuzalisha tani
milioni 3 za saruji kwa mwaka sawa na mifuko 150,000 kwa siku yenye
uzito wa kilogramu 50 na kutengeneza ajira za kudumu 1,000 na zisizo
rasmi 9,000.
Mbali na Tanzania, Dangote amewekeza pia katika
nchi nyingine 14 barani Afrika katika uzalishaji wa bidhaa hiyo muhimu
katika ujenzi wa miundombinu, baadhi ya nchi hizo ni Zambia, Ethiopia,
Senegal, Ghana n.k.
Kampuni yake ya Dangote Cement imewekeza Dola 5 bilioni za Marekani katika kujenga viwanda vya saruji barani Afrika.
Waafrika tunaweza
Mnigeria huyu ni miongoni mwa Waafrika wanaoondoa
fikra ya neno ‘mwekezaji’ lazima atoke Amerika, China, Ulaya na nchi
nyingine, lakini siyo Afrika.
Wakati Dangote akifanya hayo, hivi karibuni
Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya Biashara (Unctad) lilitoa
ripoti inayoonyesha kwamba uwekezaji wa moja kwa moja kutoka nje (FDI)
katika Bara la Afrika, umongezeka kwa asilimia 5.
Taasisi nyingine ya Kimataifa ya Ernest &
Young inayojihusisha na ukaguzi wa mahesabu, kodi na ushauri kwa
kampuni, yenye makao yake makuu jijini London Uingereza inasema
wawekezaji wa Kiafrika wanaowekeza Afrika imeongezeka kutoka watu 27
mwaka 2003 hadi 145 mwaka 2011 sawa na asilimia 17 ya wawekezaji wote wa
kigeni uliofanyika mwaka uliopita.
Utafiti huo unaonyesha kuwa miradi ya uwekezaji ya
Waafrika wenyewe katika Bara la Afrika, imeongezeka kutoka miradi 339
mwaka 2003 hadi 857 mwaka 2013 sawa na asilimia 153.
Ernest & Young pia wanasema Benki za Nigeria
na Kenya ni mifano halisi ya uwekezaji unaofanywa wawekezaji wa Afrika
na imetoa mfano pia kwa Benki ya United Bank of Africa (UBA) ya Nigeria
ambayo imewekeza katika nchi 18 barani Afrika ikiwamo Tanzania.
Utafiti wa Ernest & Young unasema ongezeko la
Waafrika wanaowekeza barani humu ni dalili ya kujiamini kwamba Waafrika
wanaweza shughuli za uwekezaji.
Post a Comment