0

LONDON, ENGLAND
ARSENE Wenger amegeukwa. Kwa sasa anatembea peke yake. Mashabiki wa Arsenal wameamua kumchachamalia kutokana na tabia yake ya ubahili huku ikiwa ni saa chache baada ya timu hiyo kupokea kipigo katika mechi ya kwanza dhidi ya Aston Villa uwanjani kwao Emirates.
Kundi la mashabiki wa timu hiyo juzi Jumapili walimwandikia barua Mtendaji Mkuu wa Arsenal, Ivan Gazidis, wakimtaka amwambie Wenger abadili sera zake kuhusu masuala ya uhamisho wa wachezaji klabuni hapo.
Wenger amepewa kiasi cha Pauni 70 milioni kwa ajili ya kununua wachezaji mastaa kukiimarisha kikosi hicho ambacho kimecheza misimu minane bila ya taji lolote.
Hata hivyo mpaka sasa hajamnunua mchezaji yeyote staa zaidi ya kumchukua bure kinda, Yaya Sanogo, kutoka Auxerre ya Ufaransa.
Mabosi wa timu hiyo pamoja na Wenger mwenyewe wamekuwa wakisisitiza kwamba wahukumiwe Septemba 2 ambayo ni siku ya mwisho ya usajili, lakini mabao mawili ya Christian Benteke na la Antonio Luna yamewachanganya mashabiki wa Arsenal baada ya kipigo cha mabao 3-1 kutoka kwa Villa Jumamosi.
Wenger alizomewa na mashabiki wa timu hiyo,  lakini kama vile haitoshi, mashabiki hao wameandika katika barua yao kwamba hasira zao zitaendelea kama hatabadilika katika sera zake za uhamisho wa wachezaji.
“Msifanye makosa, kama timu yetu haitaimarika katika namna inavyocheza kwa wiki kadhaa zijazo, kutaongezeka hasira katika majukwaa na itakuwa vigumu hali kurudi kuwa ya kawaida,” inasema sehemu ya barua ya hiyo.
“Haijawahi kutokea hali mbaya ya hewa Arsenal kwa zaidi ya miaka 30 na Bodi inaonekana kuzubaa tu wakati mambo yametoka kuwa mabaya hadi mabaya zaidi. Tuna uhakika jambo hili halitatokea tena.”
Licha ya ahadi nene za kusajili wachezaji mastaa huku akisema anafanya jitihada, tayari Wenger amepoteza fursa za kusajili mastaa kama Gonzalo Higuain, Luiz Gustavo, Marouane Fellaini, Wayne Rooney na Luis Suarez wote wameota mbawa katika orodha yake.
Kesho Jumatano, Arsenal itakuwa ugenini kucheza na Fenerbahce katika pambano la kufuzu hatua za makundi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya na endapo mambo yakiwa mabaya, Wenger atajikuta katika wakati mgumu zaidi.

Post a Comment

 
Top