0

 “Kama hawakumbuki rekodi, hilo ndilo CCM ilitakiwa wakumbuke. Kwamba sisi sera yetu tuliyokubaliana ilikuwa siyo Serikali mbili. Ni Serikali mbili kwenda Serikali Moja.. Joseph Butiku  

Dar es Salaam. Makada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Joseph Butiku na Njelu Kasaka wamesema kuwa msimamo wa chama hicho uliotokana na vikao vyake ni kuelekea Serikali moja na siyo kama kinavyoshikilia sasa kuendelea na Muundo wa Serikali Mbili.
Makada hao walitoa kauli hiyo kwa nyakati tofauti jijini Dar es Salaam hivi karibuni katika mahojiano na gazeti hili, ikiwa ni siku tatu kabla ya Bunge Maalumu la Katiba kuanza vikao vyake.
Akizungumza katika mahojiano maalumu ofisini kwake hivi karibuni, Butiku alisema kuwa uamuzi na msimamo huo wa CCM ulitolewa mwaka 1993 baada ya kuibuka kwa hoja ya Muungano wa Serikali tatu, iliyotolewa na wabunge waliounda kundi la G55.
“...Katika mazungumzo kwenye chama (CCM), baada ya kuwapo mawazo ya kuwapo mfumo wa Serikali tatu, ikawa Serikali mbili, lakini tukielekea Serikali moja. Huo ndiyo msimamo wa CCM ‘on record’, Serikali mbili kwenda moja,”alisema Butiku na kuongeza:
Kwa mujibu wa Butiku, mgogoro uliofanya CCM kukubali Serikali tatu uliojadiliwa kwenye vikao vya chama hicho mwaka 1992/93 awali ulikuwa kwa siri na hawakutaka Mwalimu Julius Nyerere ahudhurie.
“Yeye alishastaafu, lakini alijitahidi kujua kinachotokea ndani ya CCM, hawakupenda kumwambia,” alisema Butiku na kuongeza:
“Nyerere alikaa nao (CCM) na kuwauliza, lakini walimpinga. Alilia mbele yao akiuliza ili kujua sababu za kutaka Serikali Tatu, walimpinga.”
Akieleza namna Nyerere alivyopata wakati mgumu mbele ya wanaCCM, Butiku alisema: “Alipingwa kila kona, si mwenyekiti wa CCM wakati huo, si rais, makamu wake, rais wa Zanzibar hata waziri mkuu wakati huo na Spika wa Bunge wote walishakubali Serikali Tatu.
Mwishoni walikuwa kina Njelu Kasaka wakataka kwenda bungeni na kuiidhinisha. Ndiyo wakamwita Nyerere Dodoma.”
Butiku alikumbusha kuwa hoja ya sera ya Serikali mbili ndani ya CCM ni hoja ya Nyerere na ndiyo iliyowatoa CCM kwenye mpango wao wa kutaka Serikali tatu kwa wakati huo.
“Hoja ya Nyerere ndiyo iliwatoa CCM kwenye sera yao mpya ya Serikali tatu. Nyerere ndiyo alikuja akasema sera yetu (CCM), bado Serikali mbili. Ilimchukua siku mbili kuwashawishi kukubaliana naye,”alisema Butiku.
Alifafanua kuwa Nyerere hakuwapinga waliotaka Serikali tatu, lakini alihoji aliyewatuma na utaratibu walioufuata kuwasilisha hoja yao.
“Hakusema wasibadili, alisema kama wanataka CCM kuwa na sera ya kuwa na Serikali Tatu, irejeshwe kwanza kwenye chama, izungumzwe na kuwekwa kwenye sera na ilani ya uchaguzi. Alisema kama wananchi watapiga kura kuwachagua (CCM), watakuwa wameikubali,”alisema Butiku aliyefanya kazi na Nyerere kwa kipindi kirefu.
Alisema kuwa katika maisha yake, Nyerere alipinga kuvurugwa kwa utaratibu na uvunjaji wa Katiba, akionyesha hilo katika mambo mbalimbali ikiwamo suala hilo hata lililomwondoa madarakani aliyekuwa Rais wa Zanzibar, Aboud Jumbe.
“Ugomvi wake ni kutofuata utaratibu na kuvunja Katiba, hata ukimuuliza kama angekuwapo leo (Nyerere), angekujibu, sababu za kumfukuza Jumbe haikuwa mawazo ya kutaka Serikali Tatu, bali hakufuata Katiba katika kutaka Serikali Tatu, alivunja Katiba. Ugomvi wa Nyerere ulikuwa kuivunja Katiba ya nchi.”
Kuhusu madai ya CCM kwamba zinahitajika Serikali mbili zilizoboreshwa na siyo Serikali tatu zilizopendekezwa kwenye Rasimu ya Pili ya Katiba, Butiku alisema:
“Serikali mbili nani alikubali, waulize hao CCM, Serikali mbili za Nyerere zipo wapi. Serikali mbili za CCM zilizoboreshwa zipo wapi, mbona hawaelezi wanaficha, hawaweki wazi au wametoa kwenye gazeti maboresho ya Serikali mbili, sijaona? Wanayaficha, huu ni wakati wa kuficha?”
Aliongeza: “CCM  walikuwa na muda, wakati wa rasimu ya kwanza kuyatoa maboresho ya Serikali mbili, lakini wameshindwa hata sasa. Wanasiasa wanacheza na akili za Watanzania. Tume imewaambia rekebisheni haya, hawafanyi, kelele tu. Kazi kusema tatu mbaya, mbili zilizoboreshwa zipo wapi?”
Njelu Kasaka
Akiunga mkono kauli ya Butiku, mbunge wa zamani wa CCM, Njelu Kasaka aliyeendesha harakati za wabunge waliounda kundi la G55 kushinikiza Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuunda Muungano wa Serikali tatu, mwaka 1993, alisema baada ya kuona Zanzibar wana Serikali yao ndipo wabunge hao wakaamua kuidai Tanganyika na yeye ndiye aliyewasilisha hoja binafsi akilitaka Bunge kuridhia hoja yake.
“Bunge nalo lilikubali Serikali tatu, lakini Mwalimu Nyerere alipoona hivyo akazuia utekelezaji wa agizo hilo la Bunge hadi pale CCM watapokubaliana nalo kwa kuwa Sera ya CCM ilikuwa ni Serikali mbili kwenda moja,”alisema akiongeza:
“Nilipeleka mwenyewe hoja hiyo binafsi kwa Spika wakati huo akiwa Pius Msekwa na wabunge wengi waliniunga mkono na hoja yangu ya kuitaka Serikali tatu badala ya mbili ilipita.
“Mwanzo nakumbuka walipinga-pinga na wananchi waliunga mkono. Ingekuwa wanavyounga mkono sasa, nina hakika hoja hiyo ingepita bila wasiwasi.”
Kasaka alisema kuwa Mwalimu Nyerere alimuuliza Malecela aliyekuwa Waziri Mkuu: “Kwa nini mmeshindwa kumshauri Rais Mwinyi (Ali Hassan Mwinyi) hadi hoja hiyo ikapita? Kama ni hivyo basi mimi nitajitoa CCM.”
“Nyerere alisema agizo hilo litatekelezeka ila hadi akawaulize CCM kama wanataka pendekezo hilo lipite huku sera ya CCM ikiwa ni serikali mbili na wakikubali basi utekelezaji utaanza kutumika,” alisema Kasaka.
Aliongeza: “Katika ngazi ya kata CCM walikubali serikali tatu, lakini Kamati Kuu ilivyokaa ikapendekeza serikali mbili kuelekea serikali moja na uamuzi huo ulitolewa nakumbuka ilikuwa Agosti mwaka 1994.”
Kuhusu mapendekezo ya Tume ya Jaji Warioba, Kasaka alisema yako sahihi na wananchi wanatakiwa kuyaunga mkono kama ambavyo walivyowaunga mwaka 1993.

Post a Comment

 
Top