0
Dar es Salaam. Shirikisho la Jumuiya ya Madola (CGF) limetoa vibali vya wanamichezo watatu wa  Tanzania katika mchezo wa judo kushiriki kwenye Michezo ya Madola itakayofunguliwa kesho jijini Glasgow, Scotland.
Wachezaji, Gervas Chilipweli, Ahmed Magogo na Amour Kombo waliachwa kwenye msafara wa Tanzania ulioondoka nchini Jumatano iliyopita kwenda Scotland kwa kile kilichoelezwa na Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Filbert Bayi kuwa majina yao hayakuonekana CGF.
Mapema jana, Bayi ambaye yuko Scotland kwenye mkutano mkuu wa CGF ulioanza jana aliliambia gazeti hili kuwa shirikisho hilo limeridhia wanajudo hao kujumuishwa kwenye timu ya Tanzania.
“Tayari wamefanyiwa usajili ili kupokelewa kijijini na nimeshatuma taarifa wizarani, hivyo nadhani sasa wizara itashughulikia utaratibu wa safari ili kujumuika na wenzao kwenye michezo hii,” alisema Bayi.
Naibu Mkurugenzi wa maendeleo ya michezo nchini, Juliana Yasoda alisema tayari wamepata taarifa hiyo na sasa wako kwenye mchakato wa kuangalia wachezaji hao watafikaje Glasgow inapofanyika michezo hiyo.
“Tunaendelea na mchakato wa kuwasafirisha wachezaji wa judo, sambamba na kushughulikia visa ya Ikangaa (Dotto) ambayo tukifanikiwa wataondoka pamoja wakati wowote,” alisema Yasoda.
Akizungumzia hali ya wanamichezo wa Tanzania, Bayi alisema wote wako katika hali nzuri ya ushindani na wanaendelea na mazoezi chini ya makocha wao tayari kwa mashindano hayo.

Post a Comment

 
Top