0

 
Ni jambo la kawaida kwa wanafunzi wanaohitimu elimu ya msingi au sekondari kutokuwa na ustadi wa maisha hasa wa kujitegemea na kuepuka kuwa tegemezi kwa wazazi au walezi wao.
Hali hii inasababisha ongezeko la vijana wengi mitaani wasio na kazi na kubaki wakirandaranda mitaani wasijue la kufanya. Miongoni mwao, wamo wahitimu wa elimu mpaka vyuo vikuu.
Elimu isiyowezesha mhitimu kuwa na uwezo wa kujitegemea, wengi wanasema ni matokeo mabadiliko ya mara kwa mara katika mfumo wake ambao hivi sasa unaweka mkazo zaidi katika nadharia badala ya vitendo. Elimu ya nadharia haimwezezi muhitimu kuweza kujitegemea kwa kufanya shughuli kama kuwa mkulima, fundi nguo, viatu au mfanyabiashara.
Baadhi ya wadau wa elimu walioshiriki kwenye kongamano lililiofanyika Dar es Salaam kujadili mada isemayo ‘Elimu ya Tanzania, wanasema mfumo wa elimu unahitaji kuboreshwa ili uweze kuendana na matakwa ya jamii na taifa kwa jumla. Profesa wa Chuo Kikuu cha Ardhi, Alphonce Kessy anasema kitendo cha wanafunzi kuhitimu elimu ya msingi au sekondari wakiwa hawezi kujitegemea ni jambo la hatari.
Anasema elimu inayotolewa kwa wanafunzi kuanzia darasa la kwanza anafundishwa jinsi ya kulima mbogamboga au useremala kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.
Anasema shule zimeongezeka lakini vitendea kazi vya kufundishia na kujifunza bado ni vichache jambo linalorudisha nyuma ufanisi wa utoaji wa elimu kwa walimu.
“Mfumo wetu wa elimu unahitaji kuangaliwa ili mwanafunzi anapohitimu aweze kujiajiri, haina maana kuongeza shule na wanafunzi wanaojiandikisha huku ubora wa elimu ukiwa bado upo nyuma,” anasema Profesa Kessy.
Anaongeza: “Mwalimu wa zamani alikuwa mwalimu kweli, lakini leo hii amekuwa hathaminiki hivyo ni wakati wa Serikali kuhakikisha inarudisha hadhi ya mwalimu kwa kumboreshea masilahi na mazingira mazuri ya kuishi hasa mikoani.”
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Kitila Mkumbo anasema ili kuzalisha wasomi wenye weledi na wenye kushindana katika soko la ajira ni lazima kuwe na walimu makini na wanaoipenda kazi yao.
Anasema Serikali lazima iwekeze katika elimu kwani mwalimu akiwa mzuri hata mwanafunzi atamwelewa lakini ukiwa na walimu ambao siyo makini ni ngumu kupata jamii iliyoelimika.
Dk Mkumbo anasema kuna ulazima mfumo wa elimu ukatazamwa upya ili kuepuka tabaka la wanafunzi wanaoendelea kuhitimu wakiwa hawana ujuzi.
Aidha, Dk Mkumbo anawaomba Watanzania kutumia uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2015 kuchagua kiongozi ambaye atakuwa na agenda ya elimu na walioelimika.
Anasema tunahitaji kuchagua viongozi ambao watakuwa na agenda ya elimu kwani bila kuboresha sekta ya elimu nchi haitapiga hatua kutokana na kutokuwa na wataalamu wa kutosha wa kada mbalimbali.
Kauli ya washiriki
Mkazi wa jijini Dar es Salaam, Catherine Sirikwa anasema serikali inatakiwa kuweka mazingira bora ya walimu hasa wanaofundisha katika mazingira magumu.
Anasema mazingira ya vijijini bado siyo rafiki kwa walimu kutimiza majukumu yao ipasavyo, hivyo kunahitajika jitihada za makusudi kuwezesha maeneo hayo kuwa rafiki.
“Mishahara ikiboreshwa na mazingira ya kufundishia hasa ya vijijini yakiimarishwa, nina hakika kwamba walimu wataipenda kazi yao na kutekeleza kwa weledi mkubwa,” anasema Sirikwa.
Mwalimu wa Shule ya Sekondari ya Jitegemee ya jijini Dar es Salaam, Dominick Elias anasema shule za umma mara nyingi zinakosa uangalizi wa karibu ukilinganisha na shule binafsi.
Anasema katika mchakato huu wa Katiba kunahitajika kuwapo kwa kipengele kitakachowabana viongozi wa umma kupeleka nje watoto wao kusoma.
“Shule hizi za Serikali hazitaimarika endapo viongozi wataendelea kupeleka watoto wao nje ya nchi hivyo Katiba ijayo inatakiwa kuwabana watoto wao wakasoma katika shule hizi ili wawe na uchungu wa kuziboresha,” anasema Elias
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu John, tawi la Dar es Salaam, Godfrey Kisemba anasema elimu inayotolewa inatakiwa kuwajengea uwezo wa kuwawezesha kujenga viwanda vidogovidogo.
Anasema mitalaa ya elimu bado haina mbinu zinazomwezesha mwanafunzi anapohitimu anakuwa na uwezo mara baada ya kuhitimu masomo yake.
“Elimu yetu kweli bado haina mfumo thabiti kwani unaweza kuwakuta wanafunzi wamehitimu vyuo vikuu lakini hawana lolote la kufanya zaidi ya kusubiri kuajiriwa,” anasema Kisemba
Anaongeza: “Tunatakiwa kuwa na elimu ambao utabadili fikra za watu kwa kuwaandaa wanafunzi siyo waishi mijini bali vijijini ambako wataweza kuanzisha miradi kadhaa mfano ya kilimo, uvuvi au ufugaji.”
Mwanafunzi wa Kidato cha Sita wa Shule ya Sekondari ya Jitegemee, Sylvia Mkomwa anasema baadhi ya wanafunzi wanashindwa kufikia malengo yao kwa kuendekeza anasa kabla ya wakati.
Anasema kunahitajika kuwapo na semina mbalimbali hasa kwa wanafunzi wa kike kuelezea madhara yanayotokana na kuanza anasa mapema.
“Wazazi wanatakiwa kushirikiana na watoto wao kwa ukaribu katika kuelekeza na kutokuacha jukumu hilo kwa walimu pekee kwani mwisho wa siku anayebeba mzigo ni mzazi mwenyewe,” anasema Mkomwa
Anaongeza: “ Serikali iendelee kutoa elimu kwa usawa hasa vijijini ambako bado baadhi ya wazazi hawawapeleki watoto shuleni na kuwaacha nyumbani wakitekeleza majukumu ambayo si ya kwao.”

Post a Comment

 
Top