0
Dar es Salaam. Bodi ya Taifa ya Uhasibu na Ukaguzi wa Hesabu (NBAA), imesema watahiniwa wa shahada ya juu ya ukaguzi nchini CPA-(T) imeongezeka kutoka 478 mwaka 1975 na kufikia 5,646, mwaka huu.
Ongezeko hilo linatokana na matokeo ya mitihani ya NBAA iliyofanyika Mei, mwaka huu, kwa watahiniwa 1,327 kati ya 4,395 sawa na asilimia 30.2 kufaulu.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa NBAA, Profesa Mussa Assad akitangaza matokeo hayo jana Dar es Salaam, alisema watahiniwa 1,674 sawa na asilimia 40.8 watarudia somo au masomo waliyoshindwa na watahiniwa 1,394 sawa na asilimia 31.7 hawakufaulu mitihani.
Alisema katika ngazi ya mwisho (Final Stage Module F), watahiniwa 467 sawa na asilimia 28.7 kati ya 1,625 waliofanya mtihani huo wamefaulu na wengine 790 sawa na asilimia 48.7 watarudia somo moja na watahiniwa 368 sawa na asilimia 22.6 hawakufaulu.
“Watahiniwa 644 sawa na asilimia 30.5 kati ya watahiniwa 2,109 wamefaulu mtihani wa taaluma ngazi ya Module E na wengine 595 sawa na asilimia 33.5 watarudia somo moja na 870 sawa na asilimia 41.3 hawakufaulu,” alisema Assad ambaye pia ni Profesa wa Shule ya Bishara ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
“Tunafurahi kuona kuna ongezeko la ufaulu ukilinganisha na miaka minne iliyopita, lakini pia wanawake wameendelea kuongezeka, mwaka huu walikuwa asilimia 31 kati ya watahimiwa wote 4,395.”
Kuhusu mabadiliko ya mitalaa, Profesa Assad alisema NBAA imeibadili tangu mwezi uliopita na itaanza kutumika kwa mara ya kwanza Novemba, mwaka huu.
“Wanafunzi walioko katika mitalaa iliyofutwa wanatakiwa kusoma na kuelewa mfumo wa uhamaji iliyowekwa kwenye tovuti ya Bodi ili waweze kufahamu ni masomo gani wanatakiwa kujisajili katika mitalaa hiyo,” alisema.

Post a Comment

 
Top