0
Bahi. Mwenyekiti wa Kijiji cha Chonde Kata ya Makanda wilayani hapa, Daud Nhiti ameuagiza uongozi wa kijiji kumweka mahabusu Mwenyekiti wa Kitongoji cha Ng’ambo, Zebedayo Hemezi kwa kosa la kutohudhuria harambee ya kuchangia ujenzi wa zahanati.
Amri hiyo ilitolewa juzi baada ya mwenyekiti huyo wa kijiji kutoa agizo kwa wenyeviti wote wa vitongoji kujitokeza katika harambee hiyo na mwenyekiti huyo wa Ng’ambo kutofika bila ya taarifa.
Nhiti ambaye ni kiongozi katika kijiji hicho aliwaamuru wenyeviti hao kuhakikisha wanachangisha fedha kwa ajili ya ujenzi wa zahanati ya Kijiji cha Chonde kutokana na kijiji hicho kutokuwa na kituo cha huduma za afya tangu Uhuru.
Wazo la ujenzi wa zahanati katika kijiji hicho lilitolewa na Diwani wa Kata ya Makanda, Antoni Lyamunda.
Hata hivyo ,wazo hilo limedaiwa kugeuka mwiba kwa wananchi na sasa wanalalamikia kulazimishwa kuchangia ujenzi huo.
Baadhi ya wananchi walisema wamekuwa wakichangishwa michango kwa nguvu na wakati mwingine hulazimika kuuza mifugo yao kwa hasara.
Walisema kuna baadhi ya viongozi wamekuwa na tabia ya kuahidi kutoa michango kwa ajili ya shughuli za maendeleo lakini hawatimizi na matokeo yake hulazimisha wananchi ambao vipato vyao ni vidogo.
Diwani Lyamunda alisema kutokana na wakazi hao kutokuwa na huduma ya zahanati au kituo cha afya aliamua kuibua wazo hilo la ujenzi wa zahanati kwa kushirikisha wananchi ili kuishinikiza Serikali kutoa hela kwa ajili ya kuiendeleza.
Alisema pamoja na juhudi mbalimbali za kuanzisha ujenzi huo pia aliibua wazo la kufanya harambee kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa zahanati ya Chonde.
Katika harambehe hiyo iliyohudhuriwa na Mbunge wa Jimbo la Bahi, Omar Badwel (CCM), mwakilishi wa Mganga Mkuu wa hospitali ya rufaa, Ally Nyange, madiwani pamoja na wananchi wa kada mbalimbali Sh1.8 milioni ziliweza kupatikana na ahadi ilikuwa Sh9.8 milioni na kufanya jumla kuu kuwa Sh11.1 milion.
Katika harambee hiyo pia baadhi ya wananchi wa jamii ya wafugaji walichangia ng’ombe wawili na mbuzi wawili.

Post a Comment

 
Top